Wakazi wa Homa Bay walalamika kuhangaishwa na genge la Rock Boys
MTAA wa Shauri Yako mjini Homa Bay, ambao mchana huonekana kama makazi ya kawaida yenye shughuli nyingi za biashara, umegeuka kuwa kitovu cha uhalifu usiku kutokana na magenge ya vijana wanaowahangaisha wakazi.
Asubuhi, wanawake huuza maandazi, chapati na samosa kando ya barabara huku waendesha bodaboda wakisafirisha wanafunzi na wafanyakazi.
Lakini giza linapoingia, hali hubadilika kabisa.
Wakazi wanasema vijana wanaojulikana kama Rock Boys hujitokeza kutoka mafichoni na kuanza kuwapora, kuwashambulia na kuwatisha watu wanaorejea nyumbani.
Genge hilo linaundwa na vijana wenye umri wa kati ya miaka 16 na 19. Polisi wanasema baadhi yao waliacha shule, wengine wana rekodi za uhalifu huku baadhi wakikabiliwa na kesi mahakamani.
Wiki iliyopita, mwanamke aliyekuwa akitoka sokoni alishambuliwa na washukiwa hao kabla ya msamaria mwema kumuokoa.
Baadaye genge hilo lilimvamia msamaria huyo na kumkata kwa panga, hali iliyomwacha na majeraha mabaya usoni pamoja na kupoteza meno kadhaa.
Madaktari walisema atalazimika kufanyiwa upasuaji maalumu.
Tukio hilo liliwakasirisha wakazi walioungana kuwatafuta wahalifu hao.
Polisi waliingilia kati na kuanzisha operesheni iliyopelekea kukamatwa kwa vijana 40 wanaoshukiwa kuwa wanachama wa genge hilo.
Kamanda wa Polisi Kaunti ya Homa Bay Lawrence Koilem alisema baadhi ya waliokamatwa tayari wanakabiliwa na mashtaka ya wizi wa mabavu na watafikishwa mahakamani.
Kamishna wa Kaunti, Ronald Mwiwawi alieleza wasiwasi kuhusu ongezeko la vijana wanaotumia muda mwingi katika vituo vya mazoezi ya viungo kunyanyua vyuma badala ya kuwa shuleni, kisha kujiunga na magenge ya wahalifu.
Wataalamu wa maendeleo ya watoto wanaeleza kuwa ukosefu wa uangalizi wa wazazi umechangia ongezeko la magenge hayo.
Mwanasaikolojia Gloria Achieng alisema wazazi wengi hutumia muda mwingi kutafuta riziki na hivyo kuwaacha watoto chini ya ushawishi wa wenzao.
Aliongeza kuwa baadhi ya vijana hujiingiza kwenye uhalifu baada ya kutamani maisha au mali ya wengine huku wengine wakichagua kujiunga na magenge kutokana na migogoro ya kifamilia na kukosa upendo nyumbani.
Chifu wa eneo la Arujo, Bob Lang’o alisema baadhi ya wanachama wa Rock Boys walikuwa wakivuruga shughuli za shule na michezo kabla ya kuingia kwenye uhalifu mkubwa.
Pia alidai baadhi yao hulindwa na wanasiasa wanaowatumia kama walinzi katika mikutano ya kisiasa na kuwapa fedha.
Ukosefu wa taa za barabarani umeongeza tatizo hilo.
Wakazi wanasema ifikapo saa tano usiku, sehemu kubwa ya Shauri Yako huwa hatari kutembelewa. Wahalifu sasa wameanza hata kuvamia nyumba na kuiba mali za wakazi.
Kutokana na hali hiyo, wafanyabiashara wengi hufunga biashara mapema huku waendesha bodaboda wakiongeza nauli usiku kwa sababu ya hatari wanayokumbana nayo.