Penzi la dhati ni lenye nia njema na si unafiki
KATIKA dunia ya sasa ambapo mahusiano mengi yamejaa unafiki, ubinafsi, na tamaa, kutambua upendo wa kweli si jambo rahisi.
Watu wengi huingia kwenye uhusiano wakiwa na matumaini makubwa, lakini hukumbwa na machungu kwa sababu hawakujua jinsi ya kutambua dalili za upendo wa kweli mapema.
Upendo wa kweli hauonyeshwi kwa maneno matamu tu, bali kwa vitendo kila siku vinavyodhihirisha kujali, heshima, na kujitolea kwa dhati.
“Mtu kama huyo anafikiria mahitaji yako pia, si yake tu. Upendo wa kweli huambatana na kujali. Mtu anayekupenda kwa dhati atajali hali yako ya kihisia, kimwili, na kiroho,” asema mtaalamu wa masuala ya mahusiano Ben Mwembe.
Anasema mtu aliye na upendo wa kweli kwa mwingine huwa anamkubali jinsi alivyo na kusherehekea utu wake.
“Hatakushinikiza kubadilika utimize matarajio yake pekee, bali atakusaidia kuwa bora bila kukuvunja moyo. Si mtu wa kubadilika kulingana na hali au manufaa ya muda mfupi. Anakutendea vyema kila wakati,” aeleza.
Mtu mwenye upendo wa kweli hawezi kubadilisha tabia anaponyimwa anachotaka.
“Ukikosa kumpa ngono, pesa au muda wa kukutana naye, hatakukasirikia au kukuonyesha madharau. Anaheshimu mipaka yako. Hatavuka mipaka yako kimwili, kihisia au kiimani bila idhini yako,” asema mwanasaikolojia Njeri Kimani, mtaalamu wa masuala ya mapenzi.
Kulingana na Njeri, mtu aliye na mapenzi ya kweli kwa mwingine huwa anasikitika akimuudhi.
“Anaonyesha majuto ya kweli na si dharau au ujeuri unapokasirika na anajitahidi kujirekebisha anapokosea. Hatetei makosa yake na huwekeza zaidi katika mawasiliano,” asema Njeri.
Mtu kama huyo, asema, hutaka kuzungumza nawe, kuelewa hisia zako na kushiriki maisha yako ya kila siku huku akikutia moyo kukua kiroho, kitaaluma na kimaisha.
Njeri anasema upendo wa kweli ni wa pande mbili na mojawapo wa ishara zake kuu ni mtu kuruhusu mwenzake kumtunza na kumjali pia.
“Aliye na upendo wa kweli kwako atakubali mchango wako wa kumtunza pia, ana subira na ukuaji wako. Hatarajii ukue mara moja au ubadilike haraka, bali anakusubiri kwa upendo. Hatakufanyia mema kisha akukumbushe kila mara. Anafanya hivyo kwa upendo, si kwa faida ya muda mfupi,” aeleza Mwembe anaongeza kuwa mtu mwenye upendo wa kweli kwa mwingine huwa anafurahia mafanikio yake.
“Hana wivu, hana ushindani. Mafanikio yako ni furaha yake. Anakuthibitishia kuwa wewe ni wa muhimu kwake. Anakuonyesha kwa vitendo na maneno kuwa unathaminiwa,” asema.
Kwa sababu ni kawaida watu kutofautiana, anayekupenda kwa kweli huwa anajitahidi kupatana nawe haraka badala ya kushikilia ugomvi kwa muda mrefu.
“Hataki uhusiano wenu uchafuliwe kwa kisasi au chuki zisizoisha.Anakukosoa kwa upendo na pia anakubali kukosolewa. Anajifunza kutoka kwako bila kujihisi kudhalilishwa unapomkosoa. Hakulazimishii jambo lisilokufurahisha. Upendo wa kweli huheshimu hisia zako na hautumii shinikizo,” asema.
Anaongeza kuwa kamwe mtu hafai kukubali mwingine amuambie kuwa anampenda ilhali vitendo vyake vinathibitisha kinyume. Upendo wa kweli anasema huonekana, huishi, na huhisiwa.