Habari za Kitaifa

Matiang’i: Ruto akubali kuna tatizo la uongozi nchini

Na LAWRENCE ONGARO June 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

ALIYEKUWA Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i amesema Rais William Ruto anastahili kukiri kuna shida ya uongozi nchini na kuridhiana na wanasiasa wengine kwa umoja wa taifa.

Dkt Matiangí alisema kuwa njia pekee ya kuhakikisha Kenya inaelekea njia moja ni maridhiano na vijana ambao wamekuwa wakiandamana nchini wasikizwe.

Waziri huyo wa zamani alikuwa akiongea mnamo Jumapili alipohudhuria ibada ya Kanisa la PCEA mjini Thika. Aliambia serikali kuwa dhuluma dhidi ya vijana hazitasaidia ila ni kupitia mazungumzo na kutimiza ahadi.

Kwenye ibada hiyo, aliandamana na viongozi wengine akiwemo Mbunge wa Githunguri Gathoni Wamucomba ambaye alikashifu serikali kutokana na ghasia zilizoshuhudiwa kwenye maandamano ya wiki jana.

Wakati huo huo, Rais Ruto jana aliondoka nchini kwa ziara rasmi katika mataifa ya Uingereza na Uhispania anakotarajiwa kutia mikataba kadhaa ya ushirikiano wa kimaendeleo kati ya Kenya na nchi hizo za Uropa.

Kulingana na taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed majira ya asubuhi, Dkt Ruto akiwa Uingereza, atatia saini Mkataba mpya wa Ushirikiano wa Kimkakati kati ya Kenya na Uingereza utakaodumu kati ya 2025 hadi 2030.

“Mkataba huo unatarajiwa kufungua milango ya uwekezaji nchini Kenya, nafasi za ajira na kuifanya Kenya kuwa eneo bora ulimwenguni kibiashara, kiteknolojia na kiusalama,” akaeleza.

“Rais Ruto ataungana na Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer jijini London kutia saini mkataba huo wa ushirikiano uliohimiliwa katika nguzo nne za; biashara, hali ya anga, teknoloji na usalama,” Bw Mohamed akaeleza.