Habari za Kitaifa

Hali si shwari 2027, ripoti ya wakfu wa Kofi Annan yatoa tahadhari

Na STEVE OTIENO, NDUBI MOTURI July 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 4

MWAKA mmoja kabla ya Wakenya kupiga kura, ripoti mpya imeonya kuwa nchi iko katika hatari kubwa ya kushuhudia vurugu zinazohusiana na uchaguzi mkuu wa 2027 iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa.

Ripoti hiyo ya Kofi Annan Foundation inakadiria kuwa kuna uwezekano wa asilimia 81.6 wa kutokea kwa ghasia za uchaguzi.

Ingawa inasema Kenya imepiga hatua kubwa tangu ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007/2008, inaonya kuwa mizizi ya migogoro hiyo bado haijang’olewa.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, hakuna sababu moja pekee itakayochochea fujo.

Badala yake, ni mkusanyiko wa sababu mbalimbali kama vile ukosefu wa uvumilivu wa kisiasa, siasa za ukabila, ugumu wa maisha, ukosefu wa ajira kwa vijana, kupungua kwa imani kwa taasisi za umma na kuongezeka kwa makundi ya wahuni wanaotumiwa na wanasiasa.

Ripoti inapatia Kenya alama ya 43.9 katika Kielezo cha Hatari ya Uchaguzi, kiwango kilicho chini ya wastani wa cha Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara cha 51.1.

Hii inaonyesha kuwa Kenya ina taasisi imara zaidi kuliko mataifa mengi yaliyo katika hatari kubwa ya migogoro ya uchaguzi.

Hata hivyo, taasisi hizo zinaendelea kupoteza uaminifu wa wananchi kutokana na migawanyiko ya kisiasa, malalamishi ambayo hayajatatuliwa na wasiwasi kuhusu kutopendelea upande wowote kwa baadhi ya taasisi za serikali.

Ripoti inaeleza kuwa tangu uchaguzi wa 2022, mazingira ya kisiasa yamekuwa yakitawaliwa na ugumu wa maisha, maandamano dhidi ya ushuru, hasira kuhusu ufisadi na mwenendo wa polisi pamoja na maandamano ya vijana yaliyotokea nje ya miundo ya kawaida ya vyama vya kisiasa.

Kwa msingi huo, uchaguzi wa 2027 unaweza kuwa si ushindani wa urais pekee bali pia jukwaa la wananchi kudai uwajibikaji wa viongozi.

Wataalamu wa taasisi hiyo wanashauri polisi wapewe mafunzo zaidi kuhusu namna ya kudhibiti umati bila kutumia nguvu kupita kiasi na kuhakikisha wanabaki huru kisiasa.

Aidha, wanaitaka Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuchapisha mapema ratiba ya shughuli zake, utaratibu wa usajili wa wapigakura, ununuzi wa teknolojia ya uchaguzi na namna matokeo yatakavyosimamiwa ili kuondoa hofu na uvumi.

Ripoti hiyo imechapishwa wakati joto la kisiasa nchini linaendelea kupanda.

Katika miezi ya hivi karibuni, viongozi wa upinzani wamekuwa wakilalamikia mashambulizi katika mikutano yao wakidai serikali imelegeza kamba kwa makundi ya wahuni wanaofadhiliwa kisiasa.

Miongoni mwa waliodai kushambuliwa ni kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, kiongozi wa Democracy for the Citizens Party (DCP) Rigathi Gachagua na kiongozi wa DAP-Kenya Eugene Wamalwa walipokuwa wakielekea mkutano wa kisiasa Kikuyu.

Kiongozi wa People’s Liberation Party Martha Karua pia amedai kutishwa aliposhambuliwa akisimamia utekelezaji wa amri ya Mahakama Kuu katika Shule ya Msingi ya Gatoto, Mukuru kwa Reuben, Nairobi.

Kwa mujibu wa viongozi wa upinzani, matukio hayo si ya kawaida bali ni ishara kwamba mazingira ya kisiasa yanaendelea kuzorota kuelekea uchaguzi wa Agosti 10, 2027.

Jana, viongozi wa muungano wa upinzani walisema ripoti hiyo inapaswa kuwa onyo kwa serikali na IEBC kuchukua hatua mapema.

Bw Musyoka alisema uwezekano wa asilimia 81.6 wa vurugu unapaswa kuwatia wasiwasi Wakenya wote kwa sababu athari zake zitagusa uchumi na uwekezaji.

Kukataa siasa za vurugu

Alisema wawekezaji wa ndani na wa nje hufuata kwa karibu tathmini kama hizo na kwamba, hali ya kutokuwa na utulivu inaweza kuathiri maisha ya wananchi wengi.

Bi Karua alihimiza Wakenya kukataa siasa za vurugu na kuwataka polisi kutii Katiba badala ya maagizo yasiyo halali.

Alikumbusha viongozi walioko mamlakani kuwa madaraka si ya kudumu na kwamba ushindani wa kisiasa unapaswa kukubaliwa bila vitisho.

Kiongozi wa Democratic Party Justin Muturi alisema kurejea kwa makundi ya wahuni wa kisiasa kunahatarisha si demokrasia pekee bali pia uchumi na taswira ya Kenya kimataifa.

Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa ukosefu wa ajira kwa vijana na kupanda kwa gharama ya maisha sasa ni sababu kuu zinazowasukuma vijana kujiunga na makundi ya kisiasa yanayotumiwa kuzua fujo.

Tofauti na chaguzi zilizopita ambapo vurugu zilichochewa zaidi na ukabila, sasa matatizo ya kiuchumi yanatajwa kuwa kichocheo kikubwa cha maandamano na migogoro.

Ripoti inasema matukio ya hivi karibuni ya vijana wenye silaha kuvamia mikutano ya kisiasa katika maeneo kama Kisumu, Kisii, Nyahururu na Nyeri yanaonyesha kuwa matumizi ya wahuni wa kisiasa yanaanza kuwa jambo la kawaida.

Pia, imeonya kuwa hali ya kisiasa imebadilika kwa kasi.

Kulingana na utafiti wa Infotrak, iwapo uchaguzi ungefanyika sasa hakuna mgombea wa urais ambaye angepata zaidi ya asilimia 50 ya kura zinazohitajika kushinda katika duru ya kwanza.

Rais William Ruto anatajwa kupata takriban asilimia 32 pekee, jambo linaloongeza uwezekano wa duru ya pili yenye ushindani mkali.

Ripoti pia inaeleza kuwa kifo cha aliyekuwa kinara wa upinzani Raila Odinga kimeacha pengo kubwa katika siasa za upinzani.

Kutokuwepo kwake kumeibua mashindano ya uongozi, mazungumzo ya miungano mipya na kupanga upya mirengo ya kisiasa, hali ambayo inaweza kuongeza mvutano katika ngazi ya kitaifa na kaunti.

Katika kaunti, uchaguzi wa ugavana unaendelea kutajwa kuwa chanzo kikuu cha migogoro kutokana na ushindani wa kudhibiti rasilimali na nafasi za ajira.

Ripoti inasema iwapo taasisi kama IEBC, polisi na mahakama zitafanya kazi kwa uwazi, haki na usawa, Kenya inaweza kuepuka vurugu.

Lakini iwapo kutazuka mashaka kuhusu usajili wa wapigakura, ununuzi wa teknolojia ya uchaguzi au upeperushaji wa matokeo, hali hiyo inaweza kuchochea propaganda, taarifa za uongo na migogoro.

Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon amesema tume imejifunza kutokana na makosa ya chaguzi zilizopita na itasimamia uchaguzi kwa uwazi huku maajenti wa vyama wakiruhusiwa kushuhudia kila hatua ya kuhesabu kura.

Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja pia amesema polisi wameanza maandalizi mapema na hawataruhusu wahuni wala wanasiasa kuvuruga uchaguzi.

Naye Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI) Mohamed Amin ameahidi kuwa wahusika wote wa vurugu za kisiasa watachunguzwa na kufikishwa mahakamani bila kujali misimamo yao ya kisiasa.

Tume ya Uwiano na Utangamano wa Kitaifa (NCIC) nayo imeonya kuhusu ongezeko la matamshi ya uchochezi na ubaguzi wa kikabila, huku Mwenyekiti Kepha Nyamweya Omae akiwataka viongozi kutumia lugha ya kuunganisha badala ya kugawanya wananchi.