Habari za Kitaifa

Njaa yanukia zao la mahindi likikabiliwa na changamoto tele North Rift

Na BARNAS BII, VITALIS KIMUTAI July 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WIZARA ya Kilimo imeanza uchunguzi wa kina wa hali ya mashamba ya mahindi katika eneo la North Rift huku hofu ikiongezeka kuwa mavuno ya mwaka huu huenda yakapungua kwa kiwango kikubwa kutokana na ukame uliodumu kwa muda mrefu.

Ukame, uhaba wa mbolea ya kukuza mazao na kuongezeka kwa mashambulizi ya wadudu waharibifu vimeathiri maelfu ya ekari za mahindi, hali inayozua wasiwasi kuhusu utoshelevu wa chakula nchini.

Maafisa wa kilimo sasa wanatembelea mashamba katika maeneo yanayozalisha mahindi kwa wingi kukusanya taarifa kuhusu maendeleo ya mazao na kukadiria kiwango cha mavuno kinachotarajiwa.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Kilimo, tathmini hiyo inalenga kupima hali ya zao la mahindi lililokuzwa wakati wa mvua ya masika ya mwaka huu wa 2026 na kubaini iwapo uzalishaji utatosheleza mahitaji ya nchi.

Waziri wa Kaunti ya Uasin Gishu anayesimamia Kilimo, Sammin Kipkemboi Kottut, alisema wakulima wanapaswa kuwaruhusu maafisa hao kuingia mashambani ili kukusanya taarifa muhimu.

Alisema shughuli hiyo ya wiki mbili iliyoanza Jumatatu, Julai 13 itasaidia serikali kupanga hatua za kukabiliana na upungufu wa chakula endapo utajitokeza.

Mwaka wa 2024, eneo la North Rift lilizalisha takriban magunia milioni 44.8 ya mahindi na kuchangia mavuno ya kati ya magunia milioni 67 na 70.

Hata hivyo, mavuno ya mwaka huu yanatarajiwa kupungua kwa hadi asilimia 30 kutokana na mvua isiyotosha, uhaba wa mbolea na kurejea kwa viwavi jeshi.

Katika Kaunti ya Uasin Gishu, mdudu huyo tayari ameripotiwa katika maeneo ya Soy, Moiben na Kapseret.

“Mdudu huyu ameripotiwa katika baadhi ya maeneo na tunawahimiza wakulima kutoa taarifa mapema ili wapate dawa za kumdhibiti. Tatizo limeongezeka kutokana na mvua isiyoeleweka,” alisema Bw Kottut.

Aliongeza kuwa ukame umefanya mazao ya chakula na biashara kunyauka katika maeneo mengi, jambo linalotishia mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya kilimo.

Wataalamu wa kilimo wanaonya kuwa mdudu huyo ni hatari kwa sababu hushambulia mahindi katika hatua zote za ukuaji wake.

Aidha, nondo wa mdudu huyo wanaweza kuruka hadi kilomita 30 kwa usiku mmoja, hivyo kueneza mashambulizi kwa haraka kutoka shamba moja hadi jingine.

Mtaalamu wa kilimo kutoka Eldoret, Edwin Lang’at, alisema mabadiliko ya hali ya hewa yamezidisha matatizo ya wakulima.

“Mvua isiyotabirika inahatarisha mavuno ya wakulima ambao tayari wameathiriwa na magonjwa,” alisema.

Katika maeneo mengi ya Bonde la Ufa, mvua imekuwa ya kusuasua tangu Machi, jambo lililoathiri ukuaji na ukomavu wa mahindi.

Hali si tofauti katika South Rift.

Katika eneo la Trans Mara, Kaunti ya Narok, wakulima wengi walichelewa kupanda mahindi kutokana na ukame uliodumu kwa muda mrefu.

Wakulima sasa wanatarajia mavuno madogo, hali inayoweza kusababisha bei ya mahindi kupanda baadaye mwaka huu.

Festus Kiprono, mkulima kutoka Ololulunga, alisema mahindi mengi hayakufanya vizuri.

“Tunaelekea kupata hasara. Mahindi hayakukomaa vizuri na mavuno hayatatosha hata kurejesha fedha tulizowekeza katika mbegu, mbolea, kukodisha mashamba na kudhibiti wadudu,” alisema.

Mkulima mwingine kutoka Ntulele, Peter Masharen, aliitaka serikali kuwasaidia wakulima wa mahindi kama inavyowasaidia wakulima wa kahawa.

Maeneo ya Rongai na Mauche katika Kaunti ya Nakuru pamoja na Kipkelion, Kericho, nayo yameripoti hali kama hiyo.

Katibu wa Wizara ya Kilimo anayeshughulikia Kilimo, Dkt Paul Kipronoh Ronoh, alikiri kuwa mazao yameathirika katika maeneo mengi ya North Rift na South Rift.

“Tumebaini kuna uharibifu mkubwa wa mazao. Matokeo ya tathmini yatatusaidia kupanga hatua za kukabiliana na hali hiyo,” alisema.

Dkt Ronoh alisema iwapo tathmini itaonyesha kuwa uzalishaji wa mahindi hautatosheleza mahitaji ya taifa, serikali itaruhusu uagizaji wa mahindi kutoka nje ili kuzuia uhaba wa chakula.