Njaa yanukia katika jeshi serikali ikiondoa mlo wa bei nafuu
NJAA itawasakama wanajeshi kuanzia kesho Julai 1, 2025 baada ya serikali ya Rais William Ruto kuondoa mpango wa chakula cha bei nafuu katika Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF).
Kulingana na taarifa ambayo Taifa Leo ilipata nakala yake, kuanzia Julai 1, 2025 KDF itaanza kutekeleza mfumo wa Lipia-Ndio-Ule (PAYE) na kusitisha mfumo wa sasa ambapo serikali inalipia gharama kubwa ya chakula cha wanajeshi.
Hatua hiyo imeibua malalamishi miongoni mwa wanajeshi wengi, haswa maafisa wa cheo cha chini ambao wamekuwa wakitegemea pakubwa vyakula vya bei nafuu. Baadhi ya maafisa, walioficha majina yao, walisema mabadiliko hayo yatawaathiriwa kifedha, hasa wale wanaolipia mikopo.
Walielezea hofu kwamba baadhi yao watalazimika kukaa bila kula baada ya mfumo huo kuanza kutekelezwa.
Kwa miaka mingi, imekuwa mtindo kwa wanajeshi nchini Kenya na mataifa mengine ya ulimwengu, kwa maafisa wa kijeshi kufaidi kwa mipango ya chakula cha gharama nafuu.
Hata hivyo, Wizara ya Ulinzi imetetea uamuzi wa kusitishwa kwa mpango huo ikitaja haja ya kuboresha matumizi ya fedha na kutoa nafasi kwa maafisa “kupata nafasi ya kuchagua aina mbalimbali za vyakula”.
“Kupitia barua hii, utekelezaji wa mpango uliotajwa hapo huu umeratibiwa kuanza Julai 1, 2025. Kwa hivyo, maafisa wote wanahitaji kupata stakabadhi kuhusu utekelezaji wa mpango huo,” ikasema taarifa iliyotolewa Juni 23, 2025 na kutiwa saini na Mkuu wa Idara ya Bidhaa za Matumizi Brigedia Eric Nzioki.

“Matakwa yao yanatakiwa kuwasilishwa katika makao makuu kabla ya Juni 25, 2025. Zingatia kuwa pesa za hazina itakayosimamiwa na Kamati za PAYE katika vitengo mbalimbali zitatumika kudumisha mfumo huu,” stakabadhi hiyo inaendelea kusema.
Miundombinu na vifaa vilivyoko sasa katika kambi mbalimbali za kijeshi, zote zitatumika kufanikisha utekelezaji wa mfumo huo mpya.
“Mahitaji mengine yatashughulikiwa panapotokea haja ndani ya mwaka ujao wa kifedha wa 2025/26. Tafadhali zingatia na utekeleze,” taarifa hiyo inaendelea kusema.
Hii siyo mara ya kwanza kwa KDF kujaribu kuanzisha mfumo maafisa wake kulipia chakula. Majaribio ya zamani yaligonga mwamba kutokana na pingamizi kutoka kwa maafisa wa cheo cha chini.
Maafisa wakuu wa KDF wanadai kuwa mpango wa sasa wa chakula cha gharama nafuu una mianya ya kuchangia kupotea kwa pesa za umma, na hivyo kuwa mzigo kwa walipaushuru.
Ili kufanikisha utekelezaji wa mfumo huu mpya, KDF imeweka mwongozo bora wa kufanikisha mpito kutoka mfumo wa zamani na utekelezaji wa mfumo wa PAYE.
Aidha, KDF itaendesha mpango wa uhamasisho wa maafisa wote wa kijeshi ili waweze kuuelewa mfumo huo mpya.
Makamanda wa vikosi mbalimbali waliagizwa kuboresha miundomsingi katika vyumba vya maankuli katika kuanzia mwaka wa kifedha wa 2024?2025 na mwaka wa kifedha wa 2025/2026 kufanikisha wakiahidiwa fedha za kufadhili shughuli hizo.
Stakabadhi iliyotolewa Januari 17, 2025 iliagiza kubuniwa kwa kamati za usimamizi katika kambi zote za kijeshi kusimamia shughuli za vyumba vya maankuli.
Kulingana stakabadhi hiyo kamati hiyo iliwasilisha matokeo yake kwa Mkutano wa Kamati ya Makamanda wa Vikosi vya Jeshi uliofanyika Oktoba 29, 2024.