Habari

Mungatana achemkia Godhana kusema atakujia useneta akimaliza kuwa gavana

Na STEPHEN ODUOR June 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

USHINDANI mkali wa kisiasa umeibuka katika Kaunti ya Tana River baada ya Gavana Dhadho Godhana kutangaza nia yake ya kuwania kiti cha Useneta mwaka wa 2027, nafasi ambayo kwa sasa inashikiliwa na mpinzani wake wa muda mrefu, Bw Danson Mungatana.

Gavana Godhana, ambaye yuko katika hatamu yake ya pili na ya mwisho kama kiongozi wa serikali ya kaunti, ametangaza hadharani azma yake ya kuhamia Seneti, hatua ambayo tayari imechochea majibizano makali kati yake na Seneta Mungatana.

Akizungumza kwenye mikutano ya hadhara mjini Garsen na Hola, Bw Godhana alimshutumu Bw Mungatana kwa madai ya kushindwa kutekeleza jukumu kama mlinzi wa fedha na mtunzi wa sera za ugatuzi kwa mujibu wa Katiba.

Alisema kuwa Tana River inahitaji kiongozi bora zaidi anayejua wajibu wa kisheria.

“Kwa muda mrefu tumekuwa na watu wasiofaa katika Seneti. Tunahitaji mtu anayeelewa kazi ya kutunga sera, si mtu anayezurura kutoka mazishi moja hadi nyingine akieneza porojo,” akasema gavana.

Aidha, alidai kuwa, Bw Mungatana amekuwa akishirikiana na baadhi ya Madiwani kuikwamisha serikali yake kwa njama za kisiasa, akiongeza kuwa usimamizi wa serikali haupaswi kubadilishwa kuwa vita vya kibinafsi.

“Uongozi ni hoja, si umbeya na fitina. Hatuwezi kuendelea na siasa za chuki kila uchao,” alisema gavana huyo.

Kauli hizo zilikumbana na majibu makali kutoka kwa Bw Mungatana, ambaye alipuuzilia mbali azma ya Bw Godhana ya kuwania Useneta, akidai ni njia ya kujiepusha na uwajibikaji baada ya miaka kumi yaliyosheheni ubadhirifu katika uongozi wa kaunti.

“Si kwamba anakimbilia Seneti kuwatetea wananchi, anakimbilia huko kujiokoa na dhuluma alizotenda. Seneti si maficho ya magavana wabadhirifu. Ni taasisi ya heshima na uwajibikaji,” alisema Mungatana alipokuwa akiwahutubia wakazi wa Kipini.

Bw Mungatana, ambaye amewahi kuwa Mbunge na Naibu Waziri, alihoji maendeleo ya Gavana Godhana, akisema kuwa kaunti hiyo haina cha kujivunia baada ya miaka ya uongozi wake.

“Ni urithi gani anaacha nyuma? Kaunti imebaki nyuma kimaendeleo, imejaa umaskini, na yenye huduma duni. Watu wa Tana River wanastahili huduma bora zaidi,” aliongeza.

Majibizano hayo yameweka msingi wa kinyang’anyiro kikali cha Useneta ambacho wachanganuzi wa siasa wanasema kitakuwa cha kupigiwa mfano mwaka wa 2027.

Hata hivyo, duru zimedai kuwa, huenda Bw Mungatana akaamua kuwania ubunge au hata ugavana katika uchaguzi ujao

Kulingana na mchambuzi wa siasa, Dkt Halima Noor, uchaguzi huo una uzito mkubwa si tu kwa sababu ya hadhi ya wawaniaji, bali pia kutokana na miungano mipya ya kisiasa inayoibuka eneo hilo.

“Gavana Godhana ana mtandao mpana mashinani na rasilimali za kushawishi uamuzi wa wapigakura. Kwa upande mwingine, Mungatana amejiweka kama mtetezi wa uwajibikaji na anaonekana kuwa mlinzi dhidi ya ubadhirifu,” alisema Dkt Noor.

Aidha, alisema ingawa Bw Mungatana anaonekana kuwa na azma ya kutetea kiti chake, tetesi kuwa anaweza kuwania Ugavana au kurejea katika siasa za ubunge kupitia Garsen haziwezi kupuuzwa, kutegemea mazungumzo ya kisiasa na mwelekeo wa wazee wa eneo hilo.

Kwa upande wa wananchi, maoni ni tofauti. Wapo wanaoamini kuwa Mungatana ni mwakilishi makini anayewajibika, ilhali wengine wanahisi kuwa Godhana anastahili fursa nyingine kutumikia watu kwa njia tofauti.