Afisa wa polisi aliyemuua bosi wake amiminiwa risasi na wenzake na kufariki
AFISA wa polisi alipigwa risasi na wenzake Jumapili asubuhi baada ya kumuua mkubwa wake katika kituo cha polisi cha Ng’iya, Kaunti ya Siaya.
Tukio hilo lilihusisha afisa wa polisi wa cheo cha konstebo Martin Mwendwa ambaye alivunja nyumba ya bosi wake wa cheo cha koplo Bw Chesise. Baada ya uvamizi huo alimpiga risasi kwa kutumia bunduki ya G3 mara kadhaa.
Mlio huo wa risasi ulifanya polisi wengine kuingilia kati na wakampiga risasi Mwendwa alipokataa kujisalimisha.
Kamanda wa Polisi wa Gem Charles Wafula alithibitisha mauaji ya polisi hao wawili na akasema uchunguzi unaendelea kuyahusu.
“Asubuhi hii, afisa wa polisi ambaye anaishi nje ya kituo cha polisi alisikia mlio wa risasi. Baada ya kuwasili, alimpata mshukiwa akipiga risasi kiholela ndipo akawaita wenzake kutoka kituo cha Kogelo,” akasema Bw Wafula.
Walipowasili walijaribu kumkamata Mwendwa lakini akakataa. Kwa mujibu wa Bw Wafula, Mwendwa alitoroka kilomita moja kutoka alikomuua bosi wake kabla ya kuuawa akiwa bado na bastola aliyotumia kwenye uvamizi huo.
Bw Wafula alithibitisha kuwa uchunguzi umeanza kuhusu kile ambacho kilisababisha ufyatulianaji huo wa risasi ambao uliishia mauti ya maafisa hao wawili.
Aliwaomba maafisa wa polisi wawe wavumilivu na kujizuia kuua kwa kutumia bunduki zao huku akisifu mahamasisho kuhusu afya ya kiakili ambayo yamekuwa yakiendelezwa na Tume ya Huduma za Polisi Nchini (NPS).
Miili ya polisi hao ilipelekwa katika makafani ya Hospitali ya Kaunti ya Siaya.
Wenyeji nao walishangazwa na mauaji hayo, wakimrejelea Mwendwa kama mtu mtulivu ambaye alikuwa akishirikiana vyema na jamii.
“Hata alikuwa akichezea klabu ya soka ya hapa. Tumeshtushwa na kisa hiki na nina matumaini polisi watafanya uchunguzi wa kina kufahamu kilichotokea,” akasema mkazi Akech Yinda.