• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 3:23 PM
Mama asimulia mahangaiko ya bintiye aliyenajisiwa na mhudumu wa bodaboda

Mama asimulia mahangaiko ya bintiye aliyenajisiwa na mhudumu wa bodaboda

Na LAWRENCE ONGARO

FAMILIA moja eneo la Juja Farm, kaunti ya Kiambu,  inataka haki itendeke baada ya binti wao aliyenajisiwa kubaki na upweke.
Ilidaiwa muda wa miezi mitatu ambayo imepita binti hiyo amejaribu kujitoa uhai mara mbili bila mafanikio.
Ukweli wa mambo ni kwamba mnamo mwezi Desemba 2018, binti huyo aliabiri bodaboda mwendo wa saa mbili za usiku lakini mhudumu huyo wa bodaboda, alimpeleka kichakani na kumnajisi  kwa zaidi ya muda wa saa nne, kabla ya kumpeleka alikotarajia.
Baadaye alimuarifu mamake kuhusu tukio hilo.
Hatua ya haraka ilichukuliwa kwa kupiga ripoti kituo cha polisi cha Juja Farm.
Taarifa iliandikwa na akakubaliwa kwenda hospitalini ambapo ilithibitishwa kweli alinajisiwa.
Hata hivyo mamake msichana anasema hadi wa leo mshukiwa yuko mafichoni lakini anaonekana nyakati zingine.
“Mimi jambo linaloniudhi sana ni kwamba polisi wanaostahili kunisaidia wanaonekana wanamkinga mshukiwa. Ni jambo linalofanya kesi hiyo kuonekana kuwa ngumu kuendesha,” alisema mama huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe hadharani.
Anasema bintiye anasomea shule moja ya upili katika kidato cha tatu.
“Msichana wangu amesongwa na mawazo mengi ajabu ambapo kwa muda wa miezi miwili mitatu hivi iliyopita amejaribu kujitoa uhai mara mbili; jambo ambalo limepunguza bidii yake masomoni. Tafadhali ninaomba haki kutoka kwa serikali,” alijitetea mama huyo.
Uchunguzi
Naye naibu wa afisa mkuu wa polisi OCPD, kituo cha Juja, Bw Justine Njeru, alisema tayari wameanzisha uchunguzi wa kina ili kuona ya kwamba haki inatendeka.
“Tayari maafisa wangu wanaendelea kufanya uchunguzi ili kunasa mshukiwa ambaye inadaiwa yuko mafichoni,” alisema Bw Njeru.
Mama wa msichana anasema msichana wake alirudi kwa likizo fupi kutoka shuleni siku tatu zilizopita na mwanaye huyo amekuwa amejifungia kwenye nyumba akihofia kukejeliwa na wananchi.
Anazidi kueleza kuwa msichana huyo ameshindwa hata kula chakula kama kawaida.
Mama huyo amelazimika kuketi karibu na mwanaye kila Mara akimliwaza kwa kumpa ushauri.
“Hata mimi huhofia akiwa shuleni anaweza kufanya kitando kibaya akibaki pekee yake bila rafiki,” alisikitika mama huyo.
Mzazi hiyo anataka hatua ichukuliwe dhidi ya maafisa kadha wa polisi ambao anadai wanajaribu kumkinga mshukiwa ambaye angekuwa amefunguliwa mashtaka kwa sasa.

You can share this post!

TAHARIRI: Kila raia ana haki ya huduma za afya

UFISADI: Mawaziri watano wamulikwa

adminleo