Afya na Jamii

Unywaji wa kahawa waweza kukuongezea miaka mitano ya ziada ya ujana, utafiti wadai

Na PAULINE ONGAJI December 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KUNYWA hadi vikombe vinne vya kahawa kwa siku huenda kukasaidia kupunguza kasi ya uzee wa kibayolojia kwa watu wanaoishi na maradhi ya akili, utafiti mpya umeonyesha.

Matokeo ya utafiti yaliyochapishwa katika jarida la BMJ Mental Health yanaonyesha kuwa unywaji wa vikombe 3–4 kwa siku unahusishwa na urefu wa Telomere- viashiria vya seli za uzee sawa na takribani “miaka mitano ya ziada ya ujana kibayolojia” ikilinganishwa na watu wasiokunywa kahawa.

Hata hivyo, unywaji uliovuka kiwango hicho unaonekana kufuta manufaa hayo.

Cha kuvutia ni kwamba utafiti haukupata faida yoyote ya kinga kwa watu wanaokunywa zaidi ya vikombe 3–4 kwa siku, jambo linawiana na mapendekezo ya mashirika makuu ya afya, ikiwemo NHS na FDA ya Amerika.

Telomere hupungua kadiri mtu anavyozeeka. Mchakato huu ni wa kasi zaidi kwa watu walio na matatizo ya akili.

Kwa kuwa urefu wa telomere unaweza kuathiriwa na maisha ya mtu, watafiti walichunguza kama unywaji wa kawaida wa kahawa unaweza kupunguza kasi ya kupungua huko kwa watu wenye magonjwa makubwa ya akili.

Utafiti ulihusisha watu wazima 436 waliojiunga na mradi wa Norwegian Thematically Organised Psychosis kati ya 2007 na 2018 — 259 wakiwa na skizofrenia na 177 wakiwa na matatizo ya hisia.

Washiriki waliripoti kiasi cha kahawa wanachokunywa kwa siku na kugawanywa katika makundi manne: wasiotumia kahawa, wanaokunywa vikombe 1–2, 3–4, na wanaokunywa vikombe 5 au zaidi. Watafiti pia walirekodi historia ya uvutaji sigara.

Waliokunywa vikombe 5 au zaidi kwa siku walikuwa watu wakubwa zaidi kwa umri, na watu wenye skizofrenia walikunywa kahawa zaidi kuliko walio na matatizo ya hisia.

Uvutaji sigara, unaojulikana kuathiri uchakataji wa kafeini, ulikuwa wa juu, asilimia 77 ya washiriki walitambuliwa kuwa wavutaji kwa wastani wa miaka tisa. Walio kunywa vikombe 5 au zaidi walikuwa na historia ndefu zaidi ya uvutaji.

Watafiti walipima urefu wa telomere kwa kutumia seli nyeupe za damu na kugundua muundo wa “umbo la J”: wale waliokunywa vikombe 3–4 walikuwa na telomere ndefu kuliko wasiokunywa kabisa, huku kundi la wanaokunywa 5 au zaidi halikuonyesha faida hiyo.

Kwa kuwa utafiti huu ni wa uchunguzi, waandishi wanasema hauwezi kuthibitisha moja kwa moja kwamba kahawa hupunguza seli za uzee.

Pia walikosa data kuhusu aina ya kahawa, muda wa unywaji, kiwango cha kafeini na matumizi ya vinywaji vingine vyenye kafeini.