Wanahabari TZ wapigwa marufuku kutangaza ushahidi wa waathiriwa wa ghasia
DAR-ES-SALAAM, TANZANIA
VYOMBO vya Habari nchini Tanzania vimepigwa marufuku kutangaza moja kwa moja ushahidi unaotolewa na waathiriwa wa ghasia zilizotokea wakati wa uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba mwaka jana.
Amri hiyo ilitolewa na Tume huru ya kuchunguza vurugu za Oktoba 29 nchini Tanzania, iliyoundwa na Rais Samia Suluhu Hassan.
Kulingana na tume hiyo, kuchapishwa kwa taarifa zao kutawaathiri mno kwani kutawafanya wawe na msongo wa mawazo.
Hata hivyo uamuzi huo umepokelewa kwa mtazamo tofauti na wadau wa masuala ya Habari na wa afya ya akili Tanzania.
Tume hiyo inayoongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mohamed Chande Othman na kaimu wake, Jaji Mstaafu Ibrahim Juma ilitoa taarifa hizo Januari 24 ikisisitiza kuwa imechukua hatua hiyo ili kulinda usalama na faragha za waathirika hao.
Kwa mujibu wa tume hiyo, hatua hiyo imechukuliwa baada ya kuibuka kwa malalamishi kuwa taarifa binafsi za waathirika zinasambazwa mitandaoni bila idhini yao.
Profesa Juma alibainisha kuwa kusambaa kwa taarifa hizo kumesababisha baadhi ya waathirika kusumbuliwa na maombi ya mahojiano kutoka kwa vyombo mbalimbali vya habari, jambo linalowaletea msongo wa mawazo na changamoto ndani ya familia zao.
Mchambuzi wa masuala ya Habari na aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa Baraza la Habari Tanzania Kajubi Mukajanga amesema “Sijui kwa nini wamechukua uamuzi huo kwa sababu mambo yaliyotokea kipindi kile ni mambo yaliyokuwa hadharani. Kwa hivyo watu waliyaona na kuyajadili.”
Rais Samia Suluhu aliunda tume hiyo ili kutafuta chanzo cha vurugu za Oktoba 29 wakati wa uchaguzi mkuu na baada ya uchaguzi huo na katika hotuba zake amekuwa akisitiza kuwa tume hiyo ni huru na anaiamini.
Akizungumzia uamuzi wa tume hiyo mtaalamu wa afya ya akili, Saldine Kimangale alisema, “Sio wanahabari pekee, hata yale mazungumzo, yanaweza kufufua kumbukumbu za zamani, za tukio lililotokea, si lazima iwe mwanahabari awe ameripoti.”
Tume hiyo imeshakamilisha kusikiliza waathirika katika wilaya za Kinondoni, Temeke, Ilala, na Ubungo mkoani Dar es Salaam na inatarajiwa kuendelea na mikutano yake katika mikoa ya Dodoma, Shinyanga, Ruvuma, na Iringa kukusanya taarifa za matukio yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.
Ilidaiwa kuwa mamia walifariki katika maandamano hayo ya kupinga matokeo ya uchaguzi huo ambao Samia aliibuka mshindi.