Wamalwa:Hata mimi Ruto alijaribu kunirushia ndoana
KIONGOZI wa chama cha Democratic Action Party–Kenya (DAP-K), Eugene Wamalwa amezua mjadala kwa kukutana na mshirika mkuu wa Rais William Ruto na kisha kudai anawindwa na chama tawala kuelekea 2027.
Bw Wamalwa alikutana na Waziri wa Ushirika Wycliffe Oparanya na kuashiria uwezekano wao kushirikiana, kisha siku moja baadaye akadai kuwa Rais William Ruto anapanga kufufua Wizara ya Haki ili amteue kuisimamia lakini akasema hatameza chambo.
Akizungumza katika kituo cha redio cha humu nchini Alhamisi, Januari 29, 2026, Wamalwa, ambaye baada ya kukutana na Oparanya alikabiliwa na tetesi kuwa huenda akaondoka upinzani na kujiunga na serikali, alisema Rais anajaribu kumrai kwa kumpa wadhifa wa uwaziri ili ajiunge na serikali na kumuunga mkono katika Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Bw Wamalwa alisema hawezi kushawishiwa na wadhifa wowote wa uwaziri, akisisitiza kuwa tayari amewahi kuhudumu katika Baraza la Mawaziri kwa zaidi ya miaka 10.
Amewahi kuhudumu katika Wizara ya Haki, akieleza kuwa kabla ya Katiba ya 2010 kuanza kutekelezwa, yeye ndiye aliyesimamia uzinduzi wake.
“Kuna mipango ya kuunda upya Wizara ya Haki ili niteuliwe kuisimamia. Nimehudumu kama Waziri wa Haki hapo awali. Nilikuwa Waziri wa mwisho wa wizara hiyo. Chini ya uongozi wangu, Katiba ya 2010 ilizaliwa,” alisema Bw Wamalwa.
Bw Wamalwa alisisitiza kuwa hana hamu ya kujiunga na serikali, akiongeza kuwa wadhifa wa pekee anaotamani ni urais. Aidha, alidai kuwa kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka, pia anaraiwa na serikali ili ajiunge na Rais Ruto kumuunga mkono katika azma yake ya kuchaguliwa tena, lakini amekataa.
Kwa mujibu wa Bw Wamalwa, baada ya Rais kutambua kuwa amepoteza eneo la Mlima Kenya, ambalo lilikuwa nguzo muhimu ya ushindi wake wa 2022, na kwamba eneo la Nyanza haliwezi kutegemewa, sasa amemgeukia yeye na Bw Kalonzo.
Alidai kuwa kwa mujibu wa takwimu na taarifa zao za kijasusi, Rais Ruto anakadiriwa kushindwa katika uchaguzi ujao kwa takriban kura milioni mbili, kinyume na madai yake kuwa atashinda kwa tofauti ya kura milioni mbili hadi tatu mwaka wa 2027.
Bw Wamalwa alisema hatasukumwa na serikali kujiunga nayo na ataendelea kushirikiana na washirika wake katika upinzani katika azma ya kuwania kiti cha urais.
Hata hivyo, kauli hizi zimezua mdahalo kwa kuwa zilijiri baada ya mkutano wake na Waziri wa Ushirika, Wycliffe Oparanya, mmoja wa wafuasi wakuu wa serikali jumuishi, ambapo alidokeza watashirikiana kwa ajili ya umoja wa Mulembe.
Wiki iliyopita, Wamalwa pia alihudhuria hafla moja na Spika wa Bunge la Kitaifa, Moses Wetang’ula, ambaye alimhimiza aondoke upinzani na kujiunga na serikali, akisema yuko tayari ‘kumfungulia milango.’
Bw Wetang’ula pia alimualika Bw Wamalwa kuungana naye, Bw Oparanya na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi ili kufanikisha ndoto ya muda mrefu ya umoja wa jamii ya Mulembe.
Mwaka jana, Bw Wamalwa alidokeza njama hiyo, akisema Rais amekuwa akituma wajumbe kumshawishi ajiunge na serikali.
Alisema kuwa wakati mmoja, baada ya Waziri wa Afya Aden Duale kuhamishwa hadi Wizara ya Mazingira na Misitu, alipewa wadhifa wa Waziri wa Ulinzi lakini akakataa.
Mchanganuzi wa siasa Ken Ouma anasema msimu wa uchaguzi unapokaribia, tetesi za kila aina zitaibuka kila upande ukilenga kujiimarisha.
“Kinachoibua minong’ono ni kwamba huenda Oparanya alikuwa ametumwa kwa Wamalwa na Rais na kwamba kabla ya mkutano huo, kulikuwa na mazungumzo ambayo Wetang’ula alifahamu kiasi cha kumuahidi kiongozi wa DAP Kenya kuwa yuko tayari kumfungulia mlango, yaani kufanikisha kuingia kwake serikalini,” asema Ouma.