Wawaniaji 9,000 wanaosaka tiketi ya UDA kupanga foleni kumuona Ruto Jumatano
ZAIDI ya wawaniaji 9,000 walikuwa wamejisajili kufikia Jumapili kuhudhuria mkutano wa Rais William Ruto Jumatano hii katika ikulu ya Nairobi.
UDA imeanzisha vuguvugu la wawaniaji na wale ambao wanapanga kutumia tikiti ya chama hicho katika uchaguzi wa 2027 lazima wajisajili kufikia Februari 4.
Vuguvugu hilo linalenga kuimarisha umaarufu wa rais mashinani na pia kupima umaarufu wa chama katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Aidha, UDA itavuna kisiasa kutoka kwa wawaniaji ambao wanalenga kuitumia na watakuwa kwenye vuguvugu hilo.
Kando na kumvumisha rais mashinani, vuguvugu hilo pia litachochea chama kuwazia kutosimamisha wawaniaji katika baadhi ya maeneo kutokana na ushirikiano na washirika wake wapya kama vile ODM.
Mwenyekiti wa Bodi ya Uchaguzi wa UDA Anthony Mwaura jana alisema kuwa wawaniaji 9,221 wamejisajili. Alisema chama kitakamilisha usajili huo kufikia leo usiku ili kukamilisha mpango kuhusu mkutano wa Jumatano usiku.
“Wale wote ambao wamejisajili wanakaribishwa kushiriki mkutano wa vuguvugu la wawaniaji mnamo Jumatano, Februari 4, 2026 saa mbili asubuhi katika ikulu ya Nairobi,” akasema Bw Mwaura.
Kwenye notisi iliyotumwa na Bw Mwaura Januari 21, wanaosaka udiwani watajisajili kwa kulipa Sh2,000 kuhudhuria mkutano huo. Wanaosaka ubunge, useneta na kiti cha mbunge mwakilishi wa kike watalipa Sh5,000.
Watakaotumia UDA kuwania ugavana nao watalipa Sh10,000 huku watakaompinga Rais Ruto kuwania tikiti ya chama watalipa Sh100,000.
“Mkutano huo utakuwa jukwaa zuri kuzungumzia na kutekeleza mapendekezo ya kuandaa uteuzi au mchujo huru kabla ya uchaguzi,” akaongeza Bw Mwaura.
Wakati wa Kongamano la Baraza la Uongozi (NGC) ikulu ya Nairobi, wanachama wa UDA walisema wanaolenga kutumia chama wajisajili leo badala ya kusubiri kupima mkondo wa siasa za nchi.
“Iwapo mtu hatahudhuria, hatajisajili kisha waje mwaka ujao na ni wawaniaji maarufu, tutafungua mwanya wa wawaniaji kujisajili tena ama usajili huu wa Februari 4 ndio wa mwisho?” akauliza Mbunge wa Teso Kusini Mary Emase wakati wa mkutano wa ikulu.
Akimjibu Rais Ruto alisema hawajafunga dirisha la usajili lakini watafanya kazi na wale ambao wametambua chama mapema na kuanza kufanya kazi nao.
Kiongozi wa nchi alilamika kuwa baadhi ya wagombeaji huja dakika za mwisho UDA, wanashinda mchujo na wakishachaguliwa, wanaanza kuasi chama.
“Wanakuja, hawachangia chochote kwa chama kisha wanakuja kusema wanataka tikiti ya chama,” akasema Rais Ruto akisisitiza lengo lake ni kujenga UDA iwe imara kuanzia mashinani.
Rais alisema Kanu iliongoza miaka mingi kwa sababu ilikuwa na uwakilishi na nguvu mashinani, mwenendo alisisitiza uliigwa na ODM.