Habari Mseto

Serikali itapunguza bei ya mbolea na mbegu mwaka ujao, Rais aahidi

Na CECIL ODONGO August 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto ameahidi kwamba serikali itapunguza bei ya mbolea na mbegu mwaka ujao ili kutoa afueni kwa wakulima waliopata hasara mwaka huu baada ya mimea yao kunyauka kutokana na uhaba wa mvua.

Walioathirika zaidi ni wakulima wa mahindi katika eneo la Kaskazini mwa Bonde la Ufa, linalotegemewa pakubwa kwa uzalishaji wa chakula cha kukidhi hitaji la kitaifa.

“Serikali itaingilia kati kwa kupunguza bei ya mbolea na mbegu kuanzia msimu ujao wa upanzi ili kuhakikisha kuwa wakulima wanaongeza uzalishaji kufidia hasara ya mwaka huu,” akasema mnamo Jumapili alipohudhuria ibada katika kanisa la Kianglikana, Moiben, Kaunti ya Uasin Gishu.

Hata hivyo, Rais hakubainisha ni kwa kiwango kipi bei ya pembejeo hizo zitapunguzwa.

Wakati huu mbolea ya upanzi inauzwa kwa Sh2,500 kwa gunia la kilo 50, chini ya mpango wa serikali wa utoaji mbolea kwa bei nafuu.

Nayo Kampuni ya Mbegu Nchini (KSC) inauza mbegu za mahindi kwa Sh260 kwa kilo huku ikiuza gunia la kilo 25 kwa Sh6,560.