Kimataifa

RSF iliwateka watoto ikawageuza watumwa katika vita na jeshi la Sudan – Ripoti

Na REUTERS February 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

AL-FASHIR, SUDAN

KUNDI la waasi liliwateka nyara watoto lilipotwaa eneo la Al-Fashir mnamo Oktoba na katika mashambulizi mengineyo Darfur kwenye mapigano yaliyoshuhudiwa nchini Sudan, na wakati mwingine kuwaua wazazi wao, mashahidi wamesema.

Maelezo hayo kutoka kwa mashahidi kadhaa waliohojiwa na Reuters, yalijumuisha wapiganaji kutoka kwa kikosi cha Rapid Support Forces (RSF) kueleza familia kwamba watoto hao watatumiwa kama watumwa kuchunga mifugo.

RSF imekabiliana katika vita vikali na jeshi la Sudan tangu Aprili 2023, kuhusu ni upande upi utakaoendesha taifa hilo lililojaaliwa migodi tele ya madini, ardhi kubwa yenye rotuba na bandari za Bahari ya Shamu.

Japo makundi ya kutetea haki za binadamu yameripoti maovu ya kivita kutoka pande zote ikiwemo kuwasajili watoto makurutu kupigana, kuteka nyara watoto na kuwafanya watumwa, yanayohusishwa na RSF na vikosi vinavyowaunga mkono, visa hivyo havijaripotiwa hapo mbeleni na vituo vingine vya habari.

Mashahidi hao 26 walizungumza na Reuters ana kwa ana au kwa simu baada ya kukimbilia mji wa Tawila, Kaskazini mwa Darfur au Chad Mashariki.

Walisimulia kuhusu matukio 23 tofauti ambapo watoto wasiopungua 56 wenye umri kati ya miezi miwili na miaka 17 walitekwa nyara katika mashambulizi ya tangu 2023.

Sita walisimulia kuhusu jamaa zao binafsi waliotwaliwa.

Reuters haikuweza kubaini ni watoto wangapi kwa jumla wametekwa nyara. Pia ilishindwa kuthibitisha kwa njia huru masimulizi ya mashahidi au kufuatilia yaliyowasibu watoto hao baada ya kutekwa nyara.

RSF haikujibu ripoti hizo za utekaji nyara, kuwadhulumu watoto na kuwaua watoto wao.

Awali ilikanusha kuwalenga raia kimakusudi na kusema inawachunguza wapiganaji wanaotuhumiwa kuhusu dhuluma hizo.

Wataalam watatu wa sheria walisema visa hivyo vya utekaji nyara huenda vinajumuisha kufungwa jela kinyume cha sheria na mateso, na ni sawa na maovu ya kivita na uhalifu dhidi ya binadamu.

Masimulizi yaliyokusanywa na Reuters huenda vilevile yakajumuisha matendo ya utumwa na biashara ya watumwa kinyume cha sheria za kimataifa na miafaka kadhaa ya kimataifa, alisema wakili wa kimataifa aliyekuwa mshauri maalum kuhusu uhalifu wa utumwa katika Mahakama ya Kimataifa (ICC), Patricia Sellers.

Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Watoto (UNICEF), Sudan, Sheldon Yett, alisema hajapokea ripoti zozote kuhusu watoto kutekwa nyara ili kutumika kama watumwa wala kuchunga mifugo, lakini masimulizi yaliyokusanywa na Reuters “yanahuzunisha kuwa yanalingana na mtindo mpana wa dhuluma tunazozidi kuona dhidi ya watoto.”

Hakufafanua zaidi.

RSF ilibadilika kutoka kilichofahamika kama wapiganaji wa Janjaweed waliopigana pamoja na vikosi vya serikali chini ya uongozi wa aliyekuwa kiongozi wa Sudan Omar al-Bashir, na walishutumiwa kwa mauaji ya halaiki mjini Darfur katika miaka ya 2,000.

Katika machafuko hayo, Janjaweed iliwateka nyara watoto na kuwalazimisha kufanya kazi za nyumbani, kuchunga mifugo, au kufanya kazi kama watumwa wa ngono, kulingana na ripoti zilizotolewa wakati huo na makundi ya wanaharakati na watetezi wa haki za binadamu.

Jeshi la Sudan lilipoulizwa kuzungumzia masimulizi ya mashahidi kuhusu utekaji nyara wakati wa mapigano, lilisema vitendo hivyo “vinaambatana na vile vya wapiganaji wa Janjaweed katika utawala uliotangulia”.

Serikali inayoungwa mkono na Jeshi la Sudan “haiwezi kuruhusu kuwaacha raia wakiwa mateka kwa dhuluma za kikatili za waasi,” ilisema katika taarifa iliyotumiwa Reuters.