ODM ni kinyago cha Ikulu, adai Osotsi akimpiga kijembe Oburu
NAIBU Kiongozi wa ODM, Godfrey Osotsi sasa anadai kuwa chama hicho si huru kwani kinadhibitiwa moja kwa moja kutoka Ikulu ya Nairobi.
“Kile kinachofanyika ni kwamba mwelekeo wa kufuatwa na chama unafanywa na watu wa nje ndiyo maana sisi tunapinga baadhi ya maamuzi yanayotolewa,” akasema Seneta huyo wa Vihiga.
“Nimeona mikutano ikifanyika bila kufuata sheria za ndani ya chama na ndiyo maana wakati mmoja nilimwambia Rais Ruto azungumze na ODM kupitia asasi na ngazi za uongozi wa chama bali si watu binafsi,” akasema Bw Osotsi.
Kiongozi huyo ambaye amewahi kuhudumu kama mbunge mteule kupitia chama cha ANC, alisema kuwa hakuna wakati ambapo ODM iliandaa kikao na kuafikiana kuwa itaganda kwa Rais Ruto hadi 2027.
Bw Osotsi ni naibu kiongozi wa ODM, wadhifa ambao pia unashikiliwa na magavana Abdulswamaad Nassir (Mombasa) na Simba Arati (Kisii).
Bw Arati na Nassir wamekuwa wakiunga mkono chama hicho kushirikiana na UDA na kuunda muungano kabla ya uchaguzi wa 2027.
Bw Osotsi aidha alisema kiongozi wa chama hicho, Dkt Oburu Oginga ameanza kuwa na mwenendo wa kutowasikiliza viongozi wengine akimwomba pia akubali kupokea ushauri kutoka kwa wenzake kwa ajili ya umoja wa chama.
“Nina heshima sana kwa Oburu kwa sababu yeye ni kati ya wale ambao wamehudumu kwa miaka mingi bungeni. Raila hakuzungumzia siasa za 2027 na kile alichozingatia zaidi ni utekelezaji wa ajenda 10 katika muafaka na serikali,” akasema Bw Osotsi katika mahojiano na Taifa Leo.
Hata hivyo, seneta huyo alikanusha kuwa kuna pengo la uongozi ODM baada ya kifo cha Raila akisema kosa kubwa ni kwamba chama kinaongozwa vibaya tena kinyume na matarajio ya wanachama.
Ingawa hivyo, Bw Osotsi anapinga kauli ya Dkt Oginga kuwa ODM ijiunge na muungano wa kisiasa kufikia Juni mwaka huu, akisema hilo linaenda kinyume na agizo la Raila.
Alisisitiza kuwa marehemu Bw Odinga alikuwa akijali maslahi ya Wakenya ndio maana alitaka utekelezaji wa ajenda hizo 10.
Alisema wale ambao wanasema ajenda hizo zimetekelezwa wanadanganya akitaja pendekezo la kaunti kutengewa Sh450 bilioni, ahadi ambayo haijawahi kutimizwa.
Bw Osotsi alikanusha kuwa kuna mirengo tofauti ndani ya ODM akisema yanayoshuhudiwa ni maoni kinzani ambapo kundi moja linasema chama lazima kiungane na UDA na mrengo mwingine ukisisitiza chama kizingatie maslahi yake kwanza kabla ya kuingia katika muungano.
“Ni kawaida kwa watu kutofautiana kwa sababu hayo yalikuwa yakifanyika hata wakati Raila alikuwa hai. Tofauti kwa sasa ni kwamba watu hawajakaa pamoja na kuzungumzia masuala tata ndiyo maana kuna upande unaohisi unahangaishwa,” akasema Seneta huyo akionya kuwa iwapo hali itaendelea hivyo, basi ODM itawaponza wanaotaka kusikizwa chamani.
Bw Osotsi amependekeza kuwa ODM inastahili kuwa na mwaniaji wa urais badala ya kusukuma uwaniaji wa Rais Ruto kwa sababu ina viongozi ambao wamehitimu kumenyana na Rais debeni.
Anasema msukumo huo ni kwa sababu ukitathmini chaguzi nne zilizopita, basi chama kina uungwaji mkono katika nusu ya maeneo ya nchi.
Bw Osotsi alifunguka na kusema kabla ya kifo cha Raila, kulikuwa na mpango wa kuandaliwa kwa Kongamano la Kitaifa la Wajumbe wa ODM (NDC).
Anasema kongamano hilo linastahili kuandaliwa kwa kuwa wengi wanaoshikilia nyadhifa za juu ODM kwa sasa hawakuwahi kuchaguliwa.
“Hata Oburu mwenyewe ni kaimu kiongozi ndiyo maana chama kinastahili kuandaa kongamano la wajumbe kuwachagua maafisa wapya. Ni Katibu Mkuu Edwin Sifuna na Mwekahazina Timothy Bosire ambao wanashikilia nyadhifa zao kupitia uchaguzi wa chama,” akasema.
Seneta huyo amepinga vikali kuwa wanadhaminiwa na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta kuyumbisha ODM ndani kwa ndani.
“Nimeyasikia hayo baada ya madai kuzuka kuwa upande mwingine ulikuwa ukidhaminiwa na Rais Ruto,” akasema.