Habari za Kitaifa

Pigo kwa sekta ya kibinafsi serikali ikipanga kukopa Sh1 trilioni mashirika madogo nchini

Na DAVID MWERE February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MPANGO wa serikali wa kukopa Sh1 trilioni kutoka kwa mashirika ya kifedha ya humu nchini utakuwa pigo kwa sekta ya kibinafsi itakayoendelea kukosa mkopo wa gharama nafuu huku deni la serikali likitarajia kuvuka kiwango cha sasa cha Sh12.1 trilioni.

Rasimu ya Taarifa ya Sera ya Bajeti (BPS ya mwaka wa 2026) iliyoandaliwa na Hazina ya Kitaifa inaonyesha kuwa serikali inalenga kutumia Sh4.7 trilioni kama bajeti yake katika mwaka mpya wa kifedha wa 2026/27.

Lakini serikali itakabiliwa na upungufu wa Sh1.11 trilioni katika bajeti hiyo, pesa ambazo inatarajiwa kupata kwa kuchukua mkopo kutoka humu nchini na nje pamoja na ruzuku kutoka washirika wa kimaendeleo.

Ongezeko la ukopeshaji kutoka mashirika ya kifedha ya humu nchini linajiri wakati ambapo Gavana wa Benki Kuu ya Kenya (CBK) Dkt Kamau Thugge na Msimamizi wa Bajeti (CoG) Margaret Nyakang’o wameibua maswali kuhusu uwezekano wa matumizi mabaya ya pesa zitakazopatikana kutokana na mikopo na ruzuku kutoka kwa washirika wa maendeleo.

Katika rasimu hiyo ya BPS, Hazina ya Kitaifa inakisia kuwa Mamlaka ya Ushuru Nchini (KRA) itakusanya Sh3.5 trilioni katika mwaka wa kifedha wa 2026/27 na kuacha pengo karibu Sh 1.11 bilioni, ambazo ni sawa na asilimia 5.3 ya Jumla ya Utajiri wa Nchini (GDP).

Hii ni tofauti na bajeti ya sasa ya 2025/2026 ambayo ni Sh901 bilioni.

Taarifa hiyo ya sera ya bajeti inaeleza kuwa upungufu katika bajeti ya mwaka wa 2026/2027 utazibwa na mkopo wa Sh99.5 bilioni kutoka nje na mkopo wa Sh1.01 trilioni kutoka humu nchini.

“Kwa mujibu wa makadirio ya mapato na matatumizi ya pesa, upungufu wa bajeti zikiwemo ruzuku zinazotarajiwa kutoka nje ni Sh1.11 trilioni,” inasema rasimu hiyo ya BPS.

Stakabadhi kutoka Afisi ya Kutoa Ushauri kuhusu Masuala ya Bajeti Bungeni (PBO) zinasema kuwa taasisi za kifedha za humu nchini zikiwemo benki na mashirika mengine ya kutoa mikopo zinapendelea kutoa mikopo kwa serikali badala ya sekta ya kibinafsi kutokana na hakikisho ya mikopo hiyo kulipwa.

Hii ndiyo maana tangu Machi 2024 kiwango cha pesa ambazo hukopeshwa sekta ya kibinfsi kimepungua kutoka kima cha asilimia 8.1 hadi asilimia 5.7 mnamo Machi 2025.

Kulingana na PBO kiasi cha mikopo kwa sekta ya kibinafsi kimekua ilhali Biashara Ndogo Ndogo na zile za Kadri (MSMEs) ni nguzo muhimu katika ukuaji wa kiuchumi, ubunifu na uzalishaji wa nafasi za ajira.

Hapa nchini, karibu MSMEs milioni 7.4 huajiri kati ya asilimia 80 na 90 ya watu waliohitumu kuajiriwa, ikiajiri watu 15 milioni kati ya watu 18 milioni na watu 20 milioni walioajiriwa kote nchini. Kwa hivyo sekta hii huchangia asilimia 40 ya Jumla ya Utajiri wa Nchi (GDP).