Dimba

Guardiola: Bado tuna uwezo wa kuipita Arsenal tushinde EPL

Na TOTO AREGE, MASHIRIKA February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

PEP Guardiola anasema Manchester City bado wana “matumaini” ya kutwaa taji la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), licha ya kupoteza alama mbili muhimu wikendi.

City walitoka sare ya 2-2 dhidi Tottenham Hotspur ugani Tottenham Hotspur Jumapili usiku katika mechi ya EPL.

City walikuwa wanaongoza 2-0 katika kipindi cha kwanza baada ya magoli kutoka kwa Rayan Cherki na Antoine Semenyo dakika ya 11 na 44 mtawalia.

Lakini Dominic Solanke alifunga mabao mawili dakika ya 53 na 70 na kusawazishia wenyeji.

Uongozi wa Arsenal kileleni mwa jedwali na alama 53 unamaanisha kwamba, walifungua mwanya wa alama sita baada ya ushindi wa 4-0 dhidi ya Leeds Jumamosi ugani Emirates.

City wanafuata katika nafasi ya pili na alama 47 na wana safari ngumu kwenda Anfield Jumapili hii, kupambana na Liverpool (nafasi ya sita na alama 39) ambao walipata ushindi wa 4-1 dhidi ya Newcastle katika uwanja huo huo.

“Nafasi zinapokuwepo, pia matumaini yapo. Tuna matatizo katika mambo mengi, lakini wachezaji walicheza vizuri kwa kujituma,” alisema Guardiola.

Aidha, Guardiola hakuridhishwa na maamuzi ya waamuzi katika wiki chache zilizopita, na hilo anadai lilitokea tena dhidi ya Spurs.

Marudio ya goli la kwanza la Solanke yalionyesha mshambuliaji huyo alimpiga teke Marc Guéhi nyuma ya mguu wakati wa vurugu katika eneo la penalti na kulazimisha mpira kuvuka mstari.

“Ikiwa beki wa kati atamfanyia hivyo mshambuliaji ni penalti,” alisema Guardiola. Tunajifunza kwa mara nyingine tena na hili litatufanya tuwe na nguvu na bora zaidi, haswa kwa wachezaji wengi katika siku zijazo.”

Kutomakinika kwa City katika kipindi cha pili kunaleta wasiwasi kwa kikosi hicho

“Umesema kweli,” Guardiola alijibu katikia mahojiano na wanahabari baada ya mchezo. “Tulizungumza. Kama meneja, unaweza kubadilisha kitu katika kipindi cha pili. Unapocheza vibaya sana katika kipindi cha kwanza, unaweza kufanya mabadiliko ikiwa kitu hakikufanya kazi.”

Mwenzake wa Spurs Thomas Frank alisema; “Wakati wa mapumziko, nilisema mambo machache tu. Pia tulibadilisha mfumo hadi 4-4-2. Baada ya hapo, tulicheza dakika moja kwa wakati, hatua moja kwa wakati, muda mmoja kwa wakati na mwishowe tukaingia mchezoni.”

Spurs wameshinda mechi mbili tu kati ya 15 zilizopita za EPL.