Makala

Aliacha kazi ya udaktari serikalini, sasa analenga kubadilisha sekta ya afya

August 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIAKA kadhaa iliyopita, Dkt Godfrey Macharia Kiruhi alipokuwa akifanya kazi katika hospitali ya umma, alikumbana kila siku na changamoto kadhaa.

Wagonjwa walikuwa wengi, lakini madaktari na wauguzi walikuwa wachache.

Aligundua kuwa uhaba wa wataalamu wa afya ulikuwa ukisababisha msongamano mkubwa hospitalini huku wagonjwa wengi wakikosa huduma wanazohitaji kwa wakati ufaao.

Kutokana na hali hiyo, Dkt Kiruhi aliamua kuacha ajira serikalini na kuanzisha zahanati ndogo ya kibinafsi ili kuwahudumia wakazi wa eneo lake.

Kadiri mahitaji ya huduma za afya yalivyoongezeka, zahanati hiyo ilikua na hatimaye ikabadilika kuwa Hospitali ya Outspan, mojawapo ya hospitali zinazotambulika zaidi mjini Nyeri.

Hata hivyo, ukuaji wa hospitali haukuondoa changamoto zote.

Ingawa wahitimu wapya wa tiba walikuwa na maarifa ya kitaaluma, wengi wao walikosa huruma na uelewa wa mahitaji ya kihisia ya wagonjwa.

Dkt Kiruhi alitambua kuwa mageuzi ya sekta ya afya yasingewezekana bila kubadilisha mfumo wa mafunzo ya wataalamu wa tiba.

Mwaka wa 2009, alishirikiana na wadau wengine kuanzisha Chuo cha Tiba cha Outspan.

Hospitali ya Outspan iliyoanzishwa mnamo 2009. Kwa sasa hospitali hiyo imetoa fursa za ajira kwa wengi na kutoa matibabu kwa jamii. PICHA|MAKTABA

Mbali na masomo ya uuguzi na tiba, wanafunzi walilazimika kusoma saikolojia ili kuelewa hisia za wagonjwa, stadi za kidijitali za kutumia teknolojia za kisasa hospitalini pamoja na maadili ya kazi.

Mwanzoni mwa mwaka huu, taasisi hiyo ilipata kibali cha muda kutoka Tume ya Elimu ya Vyuo Vikuu (CUE) na kupandishwa hadhi kuwa Chuo Kikuu cha Outspan Global.

Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Paul Mungai Mbugua, anasema mahitaji ya kozi za afya yameongezeka kwa kiwango kikubwa.

Mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi yanafanyika katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Outspan iliyoko Nyeri.

Chuo hicho pia kinawekeza katika huduma za afya ya akili, eneo ambalo bado halijapewa uzito unaostahili nchini.

Naibu Makamu Mkuu anayeshughulikia mipango, utawala na fedha, Bw David Macharia, anasema wahitimu wa saikolojia kutoka chuo hicho hupata ajira kwa urahisi, ingawa bado jamii nyingi hazitambui umuhimu wa afya ya akili.

Kupitia Kituo cha Serenity kilichopo Nyeri, chuo hicho huendesha kampeni za uhamasishaji kuhusu matatizo ya akili na kuwapa wanafunzi nafasi ya kujifunza namna ya kuwasaidia waathiriwa wa uraibu wa dawa za kulevya na msongo wa mawazo.

Pamoja na mafanikio hayo, taasisi hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwemo uhaba wa madaktari bingwa katika nyanja kama saratani, magonjwa ya moyo na afya ya akili.

Naibu Makamu Mkuu wa masuala ya kitaaluma, Dkt Lydia Muthoni, anasema chuo hicho kimejenga ushirikiano na vyuo vikuu vya kimataifa ili kuwapa wanafunzi nafasi ya kunufaika na utaalamu wa kimataifa.

Kwa sasa, chuo hicho kina wanafunzi 1,500 na kina ndoto ya kupanua huduma zake kote nchini na baadaye katika ukanda wa Afrika Mashariki.

“Kila mwaka Wakenya wengi husafiri kwenda India kutafuta matibabu. Tunataka kubadilisha hali hiyo kwa kuimarisha huduma za afya hapa nyumbani ili wagonjwa kutoka mataifa mengine waanze kuja Kenya kutafuta matibabu,” Bw Macharia aliambia Taifa Dijitali.