Shirika lawekeza mamilioni kufanikisha mradi wa viwanda vya ngozi
Shirika la Maendeleo ya Maji la Tana Athi limewekeza Sh 330 milioni ili kuhakikisha upatikanaji wa maji ya uhakika kwa eneo la Viwanda vya Ngozi la Kinanie katika Kaunti Ndogo ya Mavoko, mradi wa serikali unaolenga kubadilisha sekta ya ngozi nchini Kenya.
Uwekezaji huo mkubwa unalenga kukidhi mahitaji ya maji ya viwandani na ya matumizi ya nyumbani ndani ya eneo hili kupitia mpango wa usambazaji maji kwa awamu.
Mpango huo unahusisha uchimbaji wa visima virefu, upanuzi wa miundomsingi ya kuhifadhi maji, pamoja na kuweka mabomba na mtandao wa ndani wa kusambaza maji.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua mradi huo Jumatatu, Afisa Mkuu Mtendaji wa Tana Athi, Bw Sammy Naporos, alisema kuwa maji pia yatasafirishwa kwa mabomba kutoka Mradi wa Maji wa Mavoko ili kuongeza kiwango cha maji.
“Maji ni rasilmali muhimu katika sekta ya ngozi. Tumeunganisha maji kutoka mji wa Athi River, umbali wa takriban kilomita 25, ili kuhakikisha upatikanaji wa maji ya kutosha na wa kudumu,” alisema.
Chini ya Awamu ya Kwanza, shirika hili linalohudumia kaunti za Makueni, Machakos, Kitui na Kajiado lilichimba na kuwezesha visima viwili virefu, likajenga tanki la chuma lililoinuliwa na likaweka bomba kuu la kilomita 2.2 na kufanya kazi za ziada kwa gharama ya Sh38.9 milioni.
Awamu ya Pili na ya Tatu, ambazo ziko katika hatua za mwisho, zilihusisha kuweka kilomita 25 za mabomba, ujenzi wa tanki la saruji pamoja na mtandao wa ndani wa usambazaji wa maji wa kilomita 5.5 kwa gharama ya Sh 292.8 milioni.
Mradi huu wa maji ni sehemu ya maendeleo mapana ya Viwanda vya Ngozi huko Kinanie kwa gharama ya Sh17 bilioni.
Eneo hili litakuwa na viwanda 36 vya ngozi, maeneo ya kuongeza thamani, biashara ndogo na kituo cha biashara. Serikali inalenga kuinua mapato ya sekta ya ngozi na kuunda maelfu ya nafasi za ajira kupitia mradi huo.