Wakenya zaidi wasaka kazi ya kujiunga na vita Ukraine licha ya maafa
UCHUNGUZI umebaini kuwa baadhi ya Wakenya wanaopigana katika vita vinavyoendelea Ukraine waliajiriwa kupitia maombi ya moja kwa moja na kampuni moja ya humu nchini, ambapo walitakiwa kurekodi video wakieleza nia yao ya kuajiriwa kama wanajeshi.
Haya yanajiri huku Mkuu wa Mawaziri, Musalia Mudavadi, akisema Ijumaa kuwa, anapanga kufanya ziara ya kidiplomasia nchini Urusi kama sehemu ya juhudi za kuwasaidia Wakenya waliokwama au kunaswa katika vita hivyo.
Stakabadhi na video zilizopatikana na Taifa Leo zinaonyesha kuwa, wengi wa walioomba kazi hiyo walikuwa maafisa wa zamani wa polisi na wanajeshi waliostaafu, waliowasilisha waziwazi sifa zao za mafunzo ya kijeshi, nidhamu na kusema walikuwa tayari kupigana, wakitaka kazi ya kijeshi nje ya nchi.
Matokeo haya ni tofauti na simulizi kwamba Wakenya hujikuta kwenye vita hivyo baada ya kudanganywa na maajenti.
Badala yake, ushahidi unaonyesha kuwepo kwa njia iliyopangwa ya uajiri, ambapo mafunzo ya awali ya kiusalama huwasilishwa kama sifa ya kuajiriwa.
Katika video kadhaa, waombaji wanaonekana wakisisitiza uzoefu wao wa kutumia silaha, historia ya operesheni na kusisitiza wako tayari kupelekwa vitani mara moja, huku wakikiri wanajua hatari za mapigano ya moja kwa moja.
Kulingana na Wizara ya Mashauri ya Kigeni, tangu 2022, shughuli za uajiri nchini Urusi zimepanuka na kujumuisha mataifa mengine ya Afrika.
Wizara hiyo ilisema katika ripoti ya mwisho wa mwaka Desemba kuwa imekuwa ikipokea maswali kutoka kwa familia kuhusu jamaa wanaodaiwa kuhusika katika vita vya Urusi na Ukraine, ikikadiria kuwa zaidi ya Wakenya 200 huenda wamejiunga na jeshi la Urusi.
Mnamo Ijumaa, Bw Mudavadi alisema serikali inakamilisha mazungumzo kuhusu Wakenya walio vitani.
“Nitafanya ziara rasmi Urusi hivi karibuni,” alisema katika mahojiano.