Habari

Maraga: Niko tayari kuungana na vinara wa Upinzani kumfanya Ruto wantam

Na KEVIN MUTAI February 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa chama cha United Green Movement (UGM) na mgombeaji urais, David Maraga, ametangaza kuwa yuko tayari kuungana na viongozi wengine wa upinzani kwa lengo la kumuondoa Rais William Ruto madarakani katika uchaguzi wa 2027.

Bw Maraga, aliyekuwa akizungumza mjini Mombasa, alisema uamuzi wake wa kushirikiana na upinzani unatokana na dhamira yake ya kukabiliana na changamoto zinazoikumba nchi, akitaja ufisadi na utamaduni wa kutojali sheria kuwa miongoni mwa matatizo makubwa.

Alisema anapigania kurejeshwa kwa misingi ya kikatiba na kuheshimiwa kwa utawala wa sheria, akionya kuwa Kenya iko hatarini kuingia kwenye mgogoro mkubwa kutokana na uporaji wa rasilmali za umma.

“Tunalenga kumuondoa Rais Ruto madarakani. Niko tayari kuungana na viongozi wanaopigania kurejesha imani ya umma na kupambana na ufisadi. Wanaopigania hayo ndio ninaowaamini, na tutaungana kwa sababu tunapigania lengo moja,” alisema.

Aidha, alilaani vikali vurugu zilizoshuhudiwa katika kanisa la ACK Witima, Othaya, wiki moja iliyopita, akiunga mkono wito wa upinzani wa maandamano ya kitaifa kudai uwajibikaji na kuchukuliwa hatua dhidi ya wahusika.

Kwa mujibu wa Bw Maraga, shambulio dhidi ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na waumini lilitekelezwa na wahuni wanaodaiwa kufadhiliwa na serikali, akitaja tukio hilo kuwa fedheha kwa taifa.

“Naunga mkono maandamano ya kitaifa kikamilifu kwa sababu hatuwezi kukubali makanisa yarushiwe vitoa machozi. Watu huenda kanisani kuomba, na polisi wanapaswa kuonyesha nidhamu,” aliongeza.

Alishutumu serikali kwa kupuuza masuala ya mazingira, hasa baada ya kuondoa marufuku ya ukataji miti iliyokuwepo tangu 2018. Maraga alisema uamuzi huo unahatarisha juhudi za uhifadhi, hasa katika maeneo kama Msitu wa Mau.

“Uharibifu wa Mau unaathiri watu wa maeneo ya nyanda za chini. Tunajua athari za mabadiliko ya tabianchi duniani, na Kenya inapaswa kuwa makini zaidi. Badala ya kuhifadhi misitu iliyosalia, tunaendelea kuiharibu,” alisema.

Wakati huo huo, chama cha UGM kinahimiza Wakenya kujisaili kama wapiga kura kwa wingi, kikirai vijana kujitokeza kwa idadi kubwa.

Viongozi wa chama hicho wanasema vijana watakuwa nguzo muhimu katika kuamua mshindi wa uchaguzi wa urais wa 2027.

“Chukueni vitambulisho vyenu na mjisajili kama wapiga kura. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuleta mabadili.ko tunayoyahitaji nchini,” alisema Bw Maraga,