Habari za Kitaifa

Kalonzo ateuliwa kiongozi mpya wa Azimio la Umoja One Kenya

Na NDUBI MOTURI February 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Rais mstaafu Uhuru Kenyatta amechukua hatua za kurejesha udhibiti wake katika upinzani  kwa kumteua Kalonzo Musyoka kiongozi mpya wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya Coalition kujaza nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na alikuwa waziri mkuu marehemu Raila Odinga.

Katika mabadiliko hayo, Mbunge wa Suba, Caroli Omondi, alipandishwa cheo kuwa katibu mkuu wa muungano huo wa upinzani kuchukua nafasi iliyoshikiliwa na mbunge wa Suna Mashariki Junet Mohammed.

Bw Junet alikuwa mshirika wa karibu wa Bw Odinga na sasa anaegemea kinara wa sasa wa chama cha ODM, Dkt Oburu Oginga.

Mabadiliko hayo ya uongozi yanaashiria mwanzo wa kupanga upya mikakati ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Maamuzi hayo yaliidhinishwa wakati wa kikao cha pamoja cha Baraza la Azimio na Kamati Kuu ya Kitaifa, kilichoongozwa na Bw Kenyatta ambaye ni mwenyekiti wa muungano huo.

Aliyekuwa karani wa Jiji la Nairobi, Philip Kisia, pia aliteuliwa kuwa mkurugenzi mtendaji wa muungano huo kuchukua wadhifa uliokuwa ukishikiliwa na aliyekuwa waziri Raphael Tuju na hivyo kukamilisha uteuzi wa viongozi watatu ambao maafisa wa chama walisema tayari majina yao yamewasilishwa katika Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa.

Katika taarifa iliyotolewa baada ya kikao hicho, Azimio ilisema mabadiliko hayo yalitokana na “mazingira ya kisiasa yanayobadilika” na yanalenga kufufua muungano, kuimarisha mshikamano wa ndani na kuupatia nguvu zaidi kitaifa.

Hata hivyo, mbali na maelezo hayo, mabadiliko hayo yanaakisi mpango wa kisiasa unaomweka Bw Kalonzo, mwanasiasa mkongwe wa upinzani na Makamu wa Rais wa zamani, katikati ya juhudi za kupatia Azimio mwelekeo mpya baada ya miezi ya kuyumba, kuhama kwa wanachama na migawanyiko ya ndani.

Kuonekana kwa Bw Kenyatta mara kwa mara ndani ya Azimio kumeonyesha dhamira yake ya kuendelea kuwa nguzo muhimu katika siasa za upinzani licha ya kuondoka madarakani mwaka 2022. Wakati wa mkutano wa hivi karibuni wa wajumbe wa chama cha Jubilee, alisisitiza kuwa chama chake kitaendelea kuwa ndani ya Azimio.

“Tutaendelea kufanya kazi, na kama chama cha Jubilee tumefanya uamuzi wa kubaki Azimio kuelekea uchaguzi wa 2027,” alisema Bw Kenyatta.

Anatarajiwa kuongoza kongamano la wawaniaji wa Muungano wa Upinzani mnamo Februari 14, hatua inayotazamwa kama jaribio la kwanza rasmi la kuupanga upya upinzani dhidi ya serikali.

Kuteuliwa kwa Bw Kalonzo si heshima ya kawaida bali ni hatua ya kimkakati inayolenga kuimarisha Azimio, kupanua mvuto wake nje ya ngome ya jadi ya Raila Odinga na kuwasilisha umoja thabiti dhidi ya utawala wa Rais William Ruto.

Uteuzi wa Caroli Omondi nao unabeba uzito mkubwa wa kisiasa. Mbunge huyo wa Suba amejitokeza kuwa mkosoaji mkubwa wa migogoro ya ndani ya ODM, hasa mrengo unaongozwa na Dkt Oburu, kaka yake Raila Odinga.

Bw Omondi amekuwa akionya kuwa ODM inakabiliwa na “mgogoro mkubwa wa ndani,” akilaumu mrengo huo kwa kupanga njama ya kuteka na kutawala Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) na kuling’anisha chama hicho na chama tawala cha UDA.

Aliwaonya vigogo wa chama akiwemo Katibu Mkuu Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi dhidi ya kuamini mchakato wa NDC.

Kupandishwa kwake cheo hadi wadhifa wenye ushawishi mkubwa wa katibu mkuu wa Azimio la Umoja One Kenya kunamuweka katikati ya usimamizi wa muungano huo.

Ingawa maafisa wa chama wametaja mabadiliko hayo kama sehemu ya juhudi za kuendeleza “uongozi jumuishi, wa misingi na unaoangalia mbele,” kwa uhalisia, yanaashiria mapambano makali yanayozidi kuongezeka kuhusu nani atadhibiti mustakabali wa upinzani na iwapo Azimio itaendelea kushirikiana na ODM.