Wafanyakazi wa kaunti wateseka hospitali zikikataa kadi ya SHA
JUMATATU iliyopita, mfanyakazi wa idara ya usafi Kaunti ya Nairobi, Miriam Ochieng, alipanga foleni nje ya hospitali ya umma eneo la Eastlands akiwa ameshika kadi yake mpya ya Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).
Hata hivyo, kufikia katikati ya asubuhi, aliarifiwa kuwa hospitali hiyo haikubali tena kadi ya SHA. Ada ya ushauri wa daktari pekee ilikuwa sawa na mshahara wake wa siku mbili.
Aliondoka bila kupokea matibabu, akiwa miongoni mwa idadi inayoongezeka ya wafanyakazi wa kaunti wanaoacha kimyakimya mpango wa afya unaodaiwa kuwa mradi mkuu wa serikali ya kaunti.
Hapo awali, Serikali ya Kaunti ya Nairobi ilikuwa imewasajili wafanyakazi wake chini ya bima ya Jubilee Health Insurance hadi mwaka 2025, ilipowahamishia kwenye mfumo wa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).
Hata hivyo, wafanyakazi sasa wanasema kwa hakika mabadiliko hayo yamewaacha bila bima ya afya.
Licha ya makato ya lazima wanayoendelea kukatwa kwenye mishahara yao, hospitali nyingi zinakataa kadi za SHA, huduma zinazotolewa ni chache na vibali huchukua muda mrefu kupatikana, hali inayozua maswali mapya kuhusu ufanisi wa mfumo mpya wa ufadhili wa afya.
Tawi la Nairobi la wafanyakazi wa Serikali za Kaunti Kenya (KCGWU), limetangaza notisi ya wiki moja kwa SHA kurekebisha kile kinachotaja kama mfumo uliogubikwa na vurugu, ambao umeacha wafanyakazi na familia zao wakihangaika kupata huduma za matibabu.
Katibu wa tawi hilo, Bw Calvin Okello, alisema Jumatatu kuwa wafanyakazi wamelazimika kutumia pesa zao binafsi kila wanapotembelea hospitali.
“Baadhi ya hospitali zimekataa kabisa kuwahudumia wafanyakazi wetu chini ya SHA. Tumepatia serikali ya kaunti notisi ya siku saba itafute bima mpya ya matibabu,” alisema Bw Okello.
Alieleza kuwa wafanyakazi walisajiliwa kwa SHA baada ya kandarasi ya awali ya bima ya matibabu ya kaunti kukamilika.
“Ni haki ya mfanyakazi kuwa na bima kamili na ya uhakika. SHA imekuwa ikifanya kazi mara kwa mara; wakati mwingine huduma zinatolewa, wakati mwingine unaambiwa hawafanyi kazi tena na SHA. Hatutaki hali hii ya kutotabirika kwa sababu inatuathiri pakubwa,” alisema.
Kwa mujibu wa chama hicho, takriban wafanyakazi 19,000 wa Kaunti ya Nairobi wanaweza kujiondoa kwenye SHA iwapo matatizo hayo hayatashughulikiwa.
“Tumesema waziwazi kuwa hatutaki SHA kwa sababu haifanyi kazi,” aliongeza.
Bw Okello alionya kuwa hali ya kutotabirika ya mpango huo imewaacha wafanyakazi katika hatari kubwa, akisema karibu watu 100,000 wakiwemo wafanyakazi na wanaowategemea wako hatarini kukosa huduma za afya.
“Hauwezi kujua kesho itakuwaje. Mfumo huu hauna uthabiti,” alisema, akiongeza kuwa pesa zinazokatwa kwenye mishahara ya wafanyakazi ni kama zinazuiliwa bila huduma.
“Ni pesa zetu, lakini unapofika hospitalini unanyimwa matibabu. Ni kama kuweka pesa benki halafu uambiwe hauwezi kuzitoa.”