Wakenya kujiunga na jeshi la Urusi kwenda kufia vitani Ukraine ni ishara ya janga la kijamii
KENYA haiko tayari kwa janga la kijamii linalosubiri taifa hili kutokana na raia wake wanaozidi kujiunga na jeshi la Urusi na kupigana katika mstari wa mbele kwenye vita vikali vinavyoendelea nchini Ukraine.
Kwa kusababisha raia wake kukata tamaa kuhusu matumaini yoyote ya kufanikiwa siku za usoni wakiwa humu nchini, serikali imewafeli raia wake inaopaswa kuwalinda kikatiba.
Miaka 62 tangu Kenya ilipojikomboa kutoka kwa ukoloni, inasikitisha kwamba wana na mabinti wa Kenya wanajipeleka kwa hiari utumwani na mautini.
Wanapofanya kazi za sulubu bila mapumziko wala malipo katika mataifa ya Kiarabu, wengine wanajiunga na magenge ya wahalifu, makundi ya kigaidi na majeshi ya kimataifa.
Kifo cha Clinton Nyapara baada ya kusajiliwa katika jeshi la Urusi kilichoripotiwa majuzi na Ukraine ni moja kati ya Wakenya ambao tayari wameangamia ng’ambo, kosa lao pekee likiwa kutafuta siku bora za usoni kwa maisha yao binafsi, familia na jamaa zao wanaowategemea.
Ungedhani vifo vya Wakenya wanaodaiwa kulaghaiwa ili kusajiliwa kujiunga na jeshi la Urusi zingewatia woga raia wenzao lakini ukweli ni tofauti kabisa.
Baadhi, wake kwa waume, sasa wanasaka namna ya kujiunga na jeshi hilo.
Wakenya wengi, hususan vijana, wameapa kutoishi kama wazazi na mababu zao na wako radhi hata kuhatarisha maisha yao iwe ni kwa kujiunga na jeshi au vinginevyo, ilmradi wakate pingu za uchochole.
Uhalisia huu unatisha lakini una mantiki ikizingatiwa Wakenya wengi ni sawa na wafu wanaotembea wakilazimika kulala mchana kutwa viwanjani, kubugia pombe haramu na mihadarati ili wajisahaulishe, angalau kwa muda mfupi, ndoto zao zilizozimwa.
Wengine huishia kufa kikatili baada ya kujiunga na makundi haramu na magenge ya wahuni yanayotumiwa na wanasiasa kutekeleza maovu yao wakati wa maandamano na msimu wa kampeni.
“Ni heri kufa ukiwa umesimama kuliko kuishi ukiwa umepiga magoti,” ni msemo maarufu unaohusishwa na kiongozi tajika wa mageuzi kutoka Mexico, Emiliano Zapata, unaomaanisha kuwa ni heri kufa kwa hadhi ukipigana na ukandamizaji kuliko kuishi utumwa.
Yamkini baadhi ya Wakenya wameuchukulia msemo huu kwa uzito zaidi na ndiyo sababu tunayoshuhudia matukio haya.
Kenya na Afrika kwa jumla inakodolea macho janga la kijamii ikizingatiwa raia wake walioshuhudia moja kwa moja maovu ya kivita mwishowe watarejea kujumuika na jamii, pasipo mikakati kabambe ya kuwadhibiti wala kushughulikia matatizo ya afya ya akili yanayozidi kuongezeka.