Habari za Kitaifa

Ripoti yaelezea wasiwasi kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Kenya

Na BENSON MATHEKA February 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HALI ya haki za binadamu nchini Kenya ilidorora mwaka uliopita, huku serikali ikikosolewa vikali kwa kukandamiza waandamanaji waliodumisha amani, wanaharakati, wanahabari na wakosoaji wa serikali, ripoti ya Human Rights Watch (HRW) inaonyesha.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, “hali ya haki za binadamu Kenya imeendelea kuwa ya kutia wasiwasi, huku ikiendeleza msako mkali dhidi ya waandamanaji wanaodumisha amani”.

HRW inasema kuwa maafisa wa usalama waliokuwa wamevaa kiraia walihusika na visa vya utekaji nyara, mateso na kutoweka kwa lazima kwa watu waliotuhumiwa kuandaa au kuunga mkono maandamano ya kupinga serikali pamoja na wanaharakati wa mitandaoni.

Ripoti hiyo inaongeza kuwa, “Serikali imefanya juhudi ndogo kuhakikisha uwajibikaji kwa ukiukaji huu na mengine mengi”, hali ambayo imeongeza hasira za umma dhidi ya serikali.

HRW inaeleza kuwa maandamano yaliendelea kushuhudiwa mwaka 2025 kutokana na sababu kadhaa, ikiwemo hasira za wananchi kuhusu nyongeza ya ushuru mwaka uliotangulia bila uwajibikaji wa matumizi ya fedha za umma.

Sababu nyingine ni kifo cha bloga na mwalimu wa shule ya upili, Albert Ojwang, akiwa kizuizini mwezi Juni, pamoja na kumbukumbu ya maandamano ya mwaka 2024.

Kwa mujibu wa HRW, “licha ya maandamano, serikali haikushughulikia ufisadi uliokita mizizi na matumizi mabaya ya rasilmali za umma, jambo lililozidi kuchochea ghadhabu ya wananchi”.

Ripoti hiyo inaeleza kwa kina madai ya ukiukaji wa haki za binadamu unaofanywa na maafisa wa usalama.

Tukio lililogusa wengi ni kukamatwa kwa Albert Ojwang na maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) Juni 7, 2025, kutokana na chapisho lililodaiwa kumkosoa Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi.

HRW inasema kuwa Ojwang alisafirishwa kwa zaidi ya saa nane hadi Kituo cha Polisi cha Central, Nairobi, ambako “kwa mujibu wa ripoti ya uchunguzi wa maiti, alifariki dunia Juni 8 kutokana na mateso”. Kifo hicho kilisababisha maandamano makubwa kote nchini.

Ripoti hiyo inaongeza kuwa, “kifo cha Ojwang ni mojawapo ya visa vingi vya mauaji, utekaji nyara, kutoweka kwa lazima na kukamatwa kiholela vilivyoripotiwa tangu maandamano ya kulalamikia gharama ya maisha ya 2023 na yale ya kupinga Mswada wa Fedha ya 2024”.

Wakati wa maandamano ya kitaifa kufuatia kifo chake, video ilienea mitandaoni ikionyesha polisi akimpiga risasi mchuuzi wa barabarani, Boniface Kariuki Mwangi.

HRW inasema kuwa polisi waliua angalau watu 31 wakati wa maandamano hayo, huku Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu ikiripoti kuwa watu 26 bado hawajulikani walipo tangu maandamano ya 2024.

Ripoti ya pamoja ya HRW na Amnesty International Kenya ya Novemba 2024, ilibaini kuwa “hakuna hata afisa mmoja wa polisi au afisa wa serikali aliyefunguliwa mashtaka kwa mauaji ya watu wasiopungua 31 wakati wa maandamano ya kulalamikia gharama ya maisha ya 2023”.

Ingawa IPOA ilisema imesajili visa 60 vya mauaji wakati wa maandamano ya 2024, HRW inasema kuwa “hakuna maelezo yaliyotolewa kuhusu uchunguzi wa visa vya utekaji nyara na kutoweka kwa lazima”.

Ripoti hiyo pia inaangazia mashambulizi dhidi ya uhuru wa kujieleza. HRW inasema kuwa, “serikali iliongeza mashambulizi ya wazi na ya siri dhidi ya wanaharakati, mashirika ya kiraia na vyombo vya habari”.

Mnamo Juni 25, 2025, Mamlaka ya Mawasiliano iliamuru vyombo vya habari kusitisha matangazo ya moja kwa moja ya maandamano na kuzima matangazo ya KTN, NTV na K24.

Zaidi ya hayo, wanahabari kadhaa walijeruhiwa wakifuatilia maandamano, huku wanaharakati wa mitandaoni wakikamatwa kiholela kwa madai ya uhalifu wa mtandao na ugaidi.

HRW pia inakosoa serikali kwa ukosefu wa uwazi katika matumizi ya ushuru mpya kama ushuru wa nyumba na bima ya afya ya kijamii.

Ripoti hiyo inasema, “hakuna mfumo wazi wa usimamizi na uangalizi wa fedha za ushuru wa nyumba wala vigezo vya wanaonufaika”.

Katika sekta ya afya, HRW inaeleza kuwa licha ya ongezeko kubwa la michango, wananchi bado wanashindwa kupata huduma bora kutokana na usimamizi mbaya na madai ya wizi wa fedha.