Habari za Kitaifa

Barua ya vinara wa Upinzani iliyozamisha Marjan wa IEBC

Na DAVID MWERE February 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BARUA ya vinara wa upinzani iliyowasilishwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuhusu kuongezwa kwa mkataba wa thamani ya mabilioni ya pesa ya mfumo wa uchaguzi wa Kenya Integrated Elections Management System (Kiems) huenda ilikuwa msumari wa mwisho uliogonga aliyekuwa Afisa Mkuu Mtendaji (CEO) wa tume hiyo, Hussein Marjan, akafutwa kazi.

Barua hiyo iliwasilishwa kwa tume hiyo Januari 28, 2026, wakati wa kikao cha alasiri kilichofanyika katika ofisi za IEBC, Anniversary Towers.

Kikao hicho kilihudhuriwa na makamishna wote wakiongozwa na Mwenyekiti Dkt Erastus Ethekon, bila kuwahusisha wanahabari wala kitengo cha mawasiliano cha IEBC.

Bw Marjan pia alihudhuria kikao hicho.

Barua hiyo, ambayo Taifa Leo imeona, inaeleza kwa kina jinsi mkataba huo wa kimkakati wa thamani ya mabilioni ya pesa, ambao kisheria unahitaji idhini ya makamishna wa IEBC katika kikao cha tume—ulivyoongezwa muda na Bw Marjan mnamo Novemba 2024 kwa kampuni ya Smartmatic ya Venezuela.

Smartmatic, ambayo imehusishwa na madai ya udanganyifu wa uchaguzi yanayohusiana na uchaguzi wa urais wa Amerika mwaka 2020, ni kampuni ya kimataifa ya teknolojia inayotoa vifaa, mifumo na huduma za michakato ya uchaguzi ikiwemo usajili wa wapiga kura, upigaji kura, kuhesabu kura na upeperushaji wa matokeo.

Wakati wa kuongezwa kwa mkataba huo, tume ya uchaguzi haikuwa na makamishna, hali inayozua maswali makubwa kuhusu ni nani aliyeidhinisha uamuzi huo, ikizingatiwa ulinzi wa kisheria uliowekwa.

Viongozi wa upinzani wanasema kuwa ununuzi wa teknolojia ya uchaguzi “sio shughuli ya kawaida kwani unagusa kiini cha demokrasia ya kikatiba ya Kenya na uthabiti wa taifa.”

“Kama ununuzi wa kimkakati, hatua za ununuzi zilipaswa kuidhinishwa na kikao cha tume. Wakati wa kuongezwa kwa mkataba huo mnamo Novemba 2024, hakukuwa na makamishna ofisini kuidhinisha ununuzi au kuongeza muda huo,” inasema sehemu ya barua hiyo.

Bw Marjan hakujibu maswali yaliyotumwa kupitia nambari yake ya simu inayojulikana, licha ya dalili zote kuonyesha kuwa aliyapokea.

Katika barua yao, upinzani ulitaka makamishna kuchukua hatua za “haraka” kuchunguza suala hilo na kuchukua hatua zinazofaa za kisheria na kiutawala, na pia “kutoa maelezo hadharani kuhusu jinsi ununuzi huo muhimu wa kimkakati ulivyoponyoka majukumu yao ya kikatiba ya usimamizi.”

Kikosi cha pamoja cha vinara wa upinzani kilichowasilisha barua hiyo kwa makamishna wa IEBC kilijumuisha viongozi wa vyama: Kalonzo Musyoka wa Wiper Patriotic Front (WPF), aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua (Democracy for the Citizens Party) na Bi Martha Karua wa People’s Liberation Party.

Wengine ni Bw Eugene Wamalwa (Democratic Action Party–Kenya), Dkt Fred Matiang’i (Jubilee Party) na Lenny Kivuti wa Devolution Empowerment Party (DEP), almaarufu Bus-Mbus.

Siku hiyo, kiongozi wa DP, Bw Justin Muturi, hakuandamana na wenzake katika upinzani kwa kuwa alikuwa akihudhuria Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) wa chama chake, uliomchagua tena na kumuidhinisha rasmi kama kiongozi na mgombea urais wa chama hicho katika uchaguzi mkuu wa 2027.

“Fedha za walipa ushuru zilipotea kwa sababu kuongezwa kwa mkataba huo ni haramu na si halali kitaratibu. Inachukuliwa kuwa teknolojia iliyotumika katika chaguzi ndogo za Novemba 27, 2025 ilitokana na hatua hiyo haramu ya mkataba,” alisema Bw Muturi, akionyesha kuunga mkono yaliyomo kwenye barua hiyo.