KAULI YA MATUNDURA: Ni kwa nini imani ya wananchi kwa Rais inadorora kila uchao?
JUZI, Naibu Rais Kithure Kindiki aliwakosoa viongozi wanaoshindwa kutimiza ahadi wanazotoa kwa raia.
Kindiki alisema, mienendo ya kuwadanganya wananchi, na baadaye kurudi kwao (kuwaomba kura?) lazima ikomeshwe mara moja.
Alisisitiza kuwa viongozi watoapo ahadi, ni sharti wahakikishe zimetimizwa kwa vitendo. Kauli ya Kindiki inasadifiana matamshi ya Rais Ruto kuhusu ufadhili wa elimu nchini.
“Kuanzia sasa, mwanafunzi yeyote, mradi tu amefaulu mtihani na kuteuliwa kujiunga na taasisi au chuo kikuu, atafadhiliwa kuafikia elimu ya juu […] sasa tuna mfumo utakaomlipia kila mwanafunzi,” akasema Dkt Ruto.
Mpaka sasa, Wakenya wengi wanatilia shaka kauli hii ya rais kwa misingi kwamba, ahadi nyingi alizowahi kutoa mbeleni hazijawahi kutimizwa mpaka sasa.
Hali hii imesababisha kupungua kwa imani ya wananchi katika serikali.
Data kutokana na asasi za Utafiti ya TIFA inadokeza kwamba, Wakenya wengi hawamwamini Rais Ruto.
Kwa nini?
Kwanza, tathmini inaonesha katika mamia ya ahadi alizotoa wakati wa kampeni kutangulia uchaguzi mkuu 2022, ni chache tu zilizokwisha kutimizwa.
Hali hii imewatamausha wananchi.
Pili, serikali inawatoza wananchi kiasi kikubwa cha ushuru.
Hatua hii inakera kwa sababu Rais alipokuwa akisaka urais, alijisawiri kama mtetezi wa wanyonge na watu wa kipato cha chini.
Alijinasibisha sana na mahasla, na kushabikiwa sana kwa mfumo wa kiuchumi wa Bottom – Up. Alivunja ahadi hii pindi alipotwaa mamlaka.
Rais anatoa ahadi za kufadhili kikamilifu wanafunzi wa vyuo vikuu katika kipindi ambapo Taasisi ya Utoaji wa Mikopo kwa wanafunzi wa Vyuo Vikuu (HELB) ina nakisi ya takriban Sh57.65 bilioni.
Kosa jingine ambalo yamkini analifanya Rais Ruto ni kujinaki kwamba kwa vyovyote vile, atashinda kwenye uchaguzi mkuu wa 2027.
Huenda hajagundua, umaarufu aliokuwa nao 2022 unapungua kila uchao kwa sababu anasema sana kuliko anavyotenda.
Katika kughairi misimamo yake mikali kuhusu sera zilizowaumiza wananchi zikiwemo kukubali kubadilisha mfumo wa ufadhili wa wanafunzi katika vyuo vikuu, yaelekea Rais Ruto anatumia mbinu ya Saikolojia kinyume (Reverse psychology).
Hii ni mbinu ya kiushawishi ambapo mtu hutetea jambo lililo kinyume kabisa na kile anachokitaka, akitarajia mtu au watu wengine kupinga pendekezo lake, na badala yake kufanya jambo unalolitaka hasa.
Kwa mfano: Ni kweli kwamba serikali haijui magenge au wahuni wanashirikiana na polisi kuhangaisha wananchi?
Itakuwa hatari kwa Rais Ruto kuendelea kutoa ahadi hewa kwenye kampeni kutangualia 2027. Utekelezaji utafaa zaidi.
Bitugi Matundura ni mhadhiri