Habari

Jaji akataza Rastafarians kuingiza bangi kortini kama ushahidi

Na RICHARD MUNGUTI February 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA kuu Jumatano, Feburuari 4, 2026 ilikataa kuruhusu Bangi almaarufu Koshopeng, Marijuana, Kaya au Mbegu kuingizwa kutolewa kama ushahidi katika kesi iliyoshtakiwa na wafuasi wa dhehebu la Rastafari.

Jaji Bahati Mwamuye alisema ijapokuwa anaombwa ahalalishe matumizi ya Koshopeng itumike kama sakaramenti ya kushusha roho mtakatifu nyakati za ibada, “huku ni kuvunja sheria.”

Jaji Mwamuye alisema Bangi au Koshopeng imeharamishwa kisheria na kamwe “hawezi kukubali kuvunja sheria kwa kuruhusu iwasilishwe kortini kama ushahidi.”

Jaji huyo alisema Bangi imetengwa kama mihadarati na “kamwe hawezi ruhusu iwasilishwe mbele yake na Rastafarians katika jitihada zao za kutaka korti iseme haki zao zinavunjwa na serikali wanaponyimwa uhuru wa kuivuta nyakati za ibada.”

Jaji huyo alisema anaelewa bayana Rastafarai wanatambua Kaya kama mojawapo ya sakaramendi bado ni haramu kwa mujibu wa sheria za Kenya.

Jaji aliwaamuru mawakili Danstan Omari na Shadrack Wambui wawasilishe picha za Koshopeng (bangi) kutoka kwa mitandao kama ushahidi katika kesi waliyowashtaki.

“Hii mahakama itaruhusu mawakili wa Rastafarai kuwasilisha picha au video kutoka kwa mitandao kama ushahidi,” alisema Jaji Mwamuye.

Wanachama wa kundi la Rastafarians wakishiriki densi nje ya mahakama ya Nairobi katika kesi wanayotaka bangi ihalalishwe. Picha|Richard Munguti

Jaji huyo alisema mahakama itaona mbegu hizo takatifu ambazo Rastafarai wanadai zinamshusha roho mtakatifu wa Mungu nyakati za ibada na “kuwabeba katika wingu juu wakiwasiliana na Muumba mbingu na nchi.”

Jaji Mwamuye alitoa agizo hilo baada ya Bw Omari kueleza korti mmoja wa walalamishi Nabii John Wambua alizuiliwa na maafisa wa polisi kuingia kortini na bangi.

Jaji huyo aliambiwa polisi walimweleza kwamba “ijapokuwa bangi hiyo ni ushahidi kwenye kesi Chama cha Marastafarai Nchini (RSK) hawawezi kumruhusu aipitishe hadi ndani ya mahakama.”

Bw Omari aliomba agizo litolewe kwa polisi wanaoshika doria katika mahakama kuu ya Milimani wawaruhusu marastafarai kuingia na “mbegu takatifu” kortini kueleza korti inavyowasaidia nyakati za ibada.

Bw Omari alilalamika kwamba wafuasi wa RSK wanasumbuliwa na polisi na kutiwa korokoroni pasipo na sababu kwa vile “wanadhaniwa kila wakati wanavuta Koshopeng.”

Mahakama iliombwa isitoe agizo lolote kwa vile hakuna ombi rasmi lililowasilishwa na Marastafarai wakiomba polisi wazimwe kuwasumbua.

Jaji Mwamuye aliahirishwa kesi hiyo hadi Machi 13 na 20 2026 itakaposikizwa.

Marastafarai wameishtaki serikali wakidai inawanyima uhuru wa kuabudu wakitumia Koshopeng.

Wanaomba serikali ishurutishwe kuwaruhusu wawe wakitumia Kaya nyakati za ibada wakisisitiza uhuru wa kuabudu ni mojawapo ya haki za kila Mkenya.