Habari

Shule taabani kwa kuchapisha picha ya mtoto bila idhini ya mzazi

Na JOSEPH WANGUI February 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SHULE za kibinafsi zinaendelea kujipata mashakani wazazi wakizishtaki kwa kutumia data za watoto wao bila idhini.
Mnamo Agosti 17, 2025, Elias*alikuwa akiendelea na shughuli zake za kila siku jijini Nairobi alipopata habari kuwa jina la mtoto wake na matokeo ya mtihani yalikuwa yamechapishwa kama tangazo gazetini.
Awali, alikuwa amepinga vikali hatua ya shule ya Nairobi Academy ya kufichua data za mtoto wake na akapewa uhakikisho kuwa jambo hilo halingefanyika.
Hata hivyo, alikuwa gazetini shule ikitangaza kufaulu kwa mtoto wake katika mtihani.
Miezi kadhaa baadaye, mvutano huo uligeuka kuwa uamuzi wa kihistoria ulioweka mfano mpya kuhusu jinsi shule nchini Kenya zinavyoshughulikia data za watoto, hususan matokeo ya mitihani ya kitaifa.
Kwa miaka mingi, shule zimekuwa zikitangaza matokeo ya wanafunzi wao na ilikuwa nadra wazazi kulalamika.
Nairobi Academy ilikanusha kuwa tangazo hilo lilikuwa la kibiashara na mnamo Januari 19, 2026, Ofisi ya Kamishna wa Ulinzi wa Data (ODPC) iliagiza Nairobi Academy kumlipa Bw Elias Sh637,500 kwa kufichua kinyume cha sheria data binafsi za mtoto kwa madhumuni ya kibiashara bila idhini ya mzazi.
ODPC iliamua kuwa matokeo ya mitihani ni data za kibinafsi.
Uamuzi huo, uliotolewa baada ya uchunguzi kubaini ukiukaji wa makusudi ni onyo kali kwa shule za binafsi zinazotumia kufaulu kwa wanafunzi kuvutia usajili.
Kamishna wa Data, Immaculate Kassait, alipata kuwa ufichuzi huo wa data ulikuwa wa kutangaza shule na ulilenga maslahi ya kibiashara ya shule kwa kuitangaza kwa wateja watarajiwa.
“Uchakataji wa data za kibinafsi za mtoto kwa madhumuni kama hayo unahitaji idhini ya wazi ya mzazi ,” alisema Kamishna katika uamuzi akibainisha kuwa idhini hiyo haikuwahi kupatikana.
Ukiukaji huo ulitokea licha ya pingamizi za awali za Elias na ahadi ya shule kutotumia data za mtoto huyo.
Uamuzi huu uliashiria mabadiliko makubwa katika jinsi shule za kibinafsi zinavyotumia picha, majina na rekodi za kitaaluma za watoto kwenye majukwaa ya umma, ikiwemo mitandao ya kijamii.
Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, ODPC imeshughulikia idadi inayoongezeka ya migogoro ambapo wazazi wanashutumu shule kwa kuchapisha picha na data za watoto kwenye mitandao ya kijamii ya TikTok, Facebook, YouTube, mabango, tovuti na magazeti, mara nyingi bila idhini na wakati mwingine licha ya pingamizi za wazi.
Kifungu cha 65(1) cha Sheria ya Ulinzi wa Data ya 2019 kinawapa haki waathiriwa wa ukiukaji kudai fidia kutoka kwa wanaosimamia au wachakataji wa data, ikijumuisha hasara ya kifedha na mateso ya kisaikolojia.
Kesi moja ilihusisha Roma School Uthiru, iliyopatiwa adhabu ya kulipa Sh4.5 milioni mnamo Agosti 2023 kwa madai ya ukiukaji wa data.
Mzazi alilalamika baada ya shule kutangaza kupitia WhatsApp mipango ya kuchapisha picha za wanafunzi TikTok kuonyesha vipaji na kuvutia wazazi kusajili watoto wao.
Wazazi walipotaka maelezo kuhusu hatua za kulinda data, hakuna yaliyotolewa. Uchunguzi ulithibitisha kuwa shule hiyo iliendesha kurasa za TikTok na Facebook zilizoonyesha picha na video za watoto.
Katika uamuzi wake, ODPC ilipata Roma School na hatia ya ukiukaji kadhaa wa Sheria ya Ulinzi wa Data, ikisisitiza kuwa idhini ya mzazi kwa uchakataji wa data za watoto ni lazima.
“Hakuna msimamizi wa data anayepaswa kuchakata data binafsi za mtoto bila idhini ya mzazi,” ilisema hukumu hiyo.
Notisi ya utekelezaji ilitolewa, na Mahakama Kuu ilikataa kuingilia kati ikitaja ukosefu wa mamlaka kuhusu kiwango cha adhabu.
Vivyo hivyo, ODPC ilichunguza Friends School Keveye Girls High School katika Kaunti ya Vihiga baada ya video ya mwanafunzi kusambaa mtandaoni.
Shule ilidai kurekodiwa kulinuiwa kwa nidhamu ya ndani na ikakana kuichapisha, lakini uchunguzi ulithibitisha kusambaa kwake mtandaoni, na kuanika mtoto kwa kejeli.
Ingawa Kamishna alithibitisha ukiukaji wa faragha.
Mnamo Juni 2024, Nova Pioneer Kenya Limited iliamriwa kulipa Sh950,000 baada ya kutumia picha ya mtoto kwenye mabango na tovuti yake bila idhini.
Mzazi aligundua picha hizo muda mrefu baada ya mtoto kuhamia shule nyingine.
“Mshtakiwa alikuwa na wajibu wa kumfahamisha mlalamishi haki za mtoto chini ya Sheria, kufichua matumizi yaliyokusudiwa ya picha, na kueleza hatua za ulinzi,” Kamishna
Huko Eldoret, Alphax Academy ilichunguzwa na ODPC kuhusu namna ilivyoshughulikia data za watoto.
Wachunguzi walibaini shule hiyo ilitumia picha za watoto kibiashara bila idhini halali na ikakosa kushirikiana na uchunguzi.
Huko Marsabit, ZAD Muslim School pia ilichunguzwa na ODPC baada ya malalamishi kuwa picha za wanafunzi zilichapishwa kwenye TikTok na YouTube kuvutia usajili.
Licha ya kukanusha, wachunguzi walithibitisha kuwa machapisho hayo yaliwaonyesha watoto wakiwa wamevaa sare za shule na yalenga maslahi ya kibiashara.
Uamuzi wa Desemba 2025 ulitaja hilo kama uuzaji mtandaoni bila idhini.
Mahakama kwa kiasi kikubwa zimeunga mkono mamlaka ya ODPC, zikithibitisha haki ya faragha ya watoto.