Habari

Matiang’i awaonya viongozi dhidi ya kufadhili wahuni

Na RUTH MBULA July 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

NAIBU Kiongozi wa Chama cha Jubilee, Dkt Fred Matiang’i, ameonya kuwa Kenya iko katika hatari kutokana na uhuni wa kisiasa.

Aliwataka viongozi kuacha kufadhili makundi ya wahuni na kukemea ghasia za kisiasa ambazo amesema zimesababisha vifo vya watu wasio na hatia katika maeneo mbalimbali nchini.

“Katika historia ya siasa za Kenya hatujawahi kushuhudia kiwango hiki cha vurugu za kisiasa zikifanywa na viongozi wanaohusishwa na serikali,” alisema.

Dkt Matiang’i alitoa kauli hiyo alipozuru maeneo ya Keumbu katika eneo la Nyaribari Chache, Gionseri, Bobasi na Nyamokenye, Kaunti ya Kisii.

Alisema siasa hazipaswi kuwagawanya Wakenya na kwamba wanaofadhili makundi ya wahuni wanapaswa kukumbuka kuwa Kenya lazima ibaki na umoja kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa 2027.

Akirejelea uzoefu wake alipokuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Matiang’i alihoji kwa nini serikali imeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kikatiba wa kulinda maisha na mali ya wananchi.

“Serikali ina rasilimali za kutosha na taarifa za kijasusi za kufuatilia, kusaka na hata kuteka wakosoaji wa kisiasa, lakini inadai haina uwezo wa kuwazuia wahuni wanaotembea hadharani wakiwa na silaha kuwashambulia wananchi,” alisema.

Aliongeza kuwa mashambulizi hayo hayawezi kutokea bila viongozi wa usalama wa eneo husika kujua au kuhusika.

Pia aliwaonya wanasiasa wanaowaajiri na kuwatuma wahuni kufanya mashambulizi akisema wanacheza mchezo hatari ambao utawageukia siku zijazo.

“Vurugu zikizidi na kushindwa kudhibitiwa, wale wahuni mnaolea watawageukia. Hakuna atakayekuwa salama, hata walio madarakani wenye ulinzi mkali,” alisema.

Dkt Matiang’i aliwahimiza wananchi na viongozi wa dini kukataa fedha za kisiasa na “fedha zilizochafuliwa na damu” zinazotumiwa kuwashawishi vijana kujiunga na makundi ya wahuni.

Akizungumzia mashambulizi yaliyotokea Keumbu wiki mbili zilizopita, alisema ameunda timu ya mawakili na wataalamu wa teknolojia kukusanya ushahidi na taarifa zitakazotumika kushtaki waliohusika.

Alisema timu hiyo inachambua video za shambulio hilo ili kubaini wahusika pamoja na wafadhili wao wa kisiasa na kuhakikisha wanachukuliwa hatua za kisheria.

“Nimekuja Keumbu kulaani vikali vitendo vya uvunjaji sheria dhidi ya Wakenya wasio na hatia. Ninawasihi watu wa Gusii kudumisha uvumilivu ambao ndio msingi wa demokrasia yetu,” alisema.

Dkt Matiang’i alitembelea Keumbu ambako viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi walivamiwa wiki mbili zilizopita katika tukio lililosababisha kuuawa kwa Vincent Osiemo maarufu kama Mapinduzi.

Baadaye alihudhuria mazishi ya Osiemo huko Gionseri, Bobasi, ambako alitoa wito wa umoja miongoni mwa jamii ya Wagusii.

Aidha, alisema uchaguzi mdogo wa Ol Kalou umefungua ukurasa mpya katika siasa za Kenya.

“Nmpongeza ndugu yangu Rigathi Gachagua, chama cha DCP, hasa Seneta Methu na timu yake ya Ol Kalou, kwa ushindi huo wa kihistoria,” alisema.