Ni vita vya ubabe ODM Oburu akimjibu Sifuna
MASWALI kuhusu uhalali wa uongozi mpya wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM), chanzo cha mamilioni ya fedha yanayotumika katika misururu ya mikutano mashinani, pamoja na mipango ya makubaliano ya uchaguzi wa 2027 na Rais William Ruto, yamekumba chama hicho chenye umri wa miaka 20.
Kifo cha nguzo yake Raila Odinga miezi mitatu iliyopita kimesababisha makundi mawili pinzani, kila moja likidai kushikilia misingi na kuendeleza itikadi za chama.
Kundi moja linaongozwa na kaka mkubwa wa Raila, Dkt Oburu Oginga, ambaye ni kiongozi wa chama, likijumuisha manaibu viongozi wa chama Simba Arati na Abdulswamad Nassir, mwenyekiti Gladys Wanga, Mbunge wa Suna Mashariki Junet Mohammed, miongoni mwa wengine.
Kundi hili limekuwa likizunguka nchi nzima kurai wanachama kupitia mikutano chini ya kaulimbiu ya ‘Linda Ground’ (Linda ngome).
Kundi jingine linaongozwa na Katibu Mkuu Edwin Sifuna, Naibu Kiongozi wa Chama na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, Gavana wa Siaya James Orengo, na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, miongoni mwa wengine.
Nalo limeanzisha mikutano sambamba iliyopewa jina ‘Linda Mwananchi’.
Ijumaa, Dkt Oginga alitoa taarifa kali akijibu mashambulizi, akisema Bw Sifuna amekuwa akiwachanganya wanachama wa chama mara kwa mara kila anapojitokeza kwenye vyombo vya habari kwa mahojiano.
“Wakati Sifuna alipouliza uhalali wa baadhi ya maafisa wa kitaifa kwa msingi kwamba walichaguliwa na Baraza Kuu la Kitaifa, alipuuza ukweli wa msingi kwamba yeye mwenyewe alichaguliwa kuwa Katibu Mkuu na kamati hiyo mnamo Februari 2018 na alitekeleza majukumu ya ofisi hiyo kikamilifu hadi Februari 2022, wakati Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe ulipomuidhinisha baadaye,” alisema Dkt Oginga.
Kiongozi huyo wa chama alikuwa akijibu kauli za Bw Sifuna katika mahojiano ya runinga ya Citizen TV Jumanne, ambapo alihoji maamuzi kadhaa ya chama, yakiwemo uhalali wa uongozi wa chama.
“Mahojiano hayo pia yalikuwa na madai yaliyopotosha umma kuhusu uhalali wa baadhi ya maafisa wa chama. ODM, tangu kuasisiwa kwake, imekuwa ikizingatia katiba yake na utawala wa sheria. Kanuni hiyo hiyo ndiyo iliyomweka kila mtu katika nafasi yake halali, akiwemo Sifuna,” Dkt Oginga alimwambia Bw Sifuna.
“Mnamo Julai 2025, alisema kuwa ODM haiwezi kungoja hadi 2027 kuamua mkakati wake baada ya uchaguzi. Leo, anauliza kwa nini kuna haraka ya kuanzisha mazungumzo na washirika watarajiwa kabla ya uchaguzi,” aliongeza.
Dkt Oginga alimkumbusha Bw Sifuna kuwa sera za ODM haziundwi kwa mapendeleo ya mtu binafsi, bali kupitia mijadala iliyopangwa na vyombo halali vya chama.
“Katibu Mkuu wakati mwingine ameshindwa kutofautisha kati ya maoni yake binafsi na sera rasmi ya chama kama inavyoamuliwa na vyombo vyetu vinavyotambuliwa kikatiba. Hili, bila shaka, limesababisha mkanganyiko miongoni mwa wanachama na wafuasi,” alisema.
Katika mahojiano hayo, Bw Sifuna alisema uteuzi wa Dkt Oginga kama kiongozi wa chama haukufuata taratibu wala masharti ya katiba ya chama.
“Kuteuliwa kwa Oburu Oginga kama kiongozi wa mpito wa chama hakukuwa kwa mujibu wa taratibu za katiba. Ushauri wangu ungekuwa, kama ningekuwapo katika mkutano huo, ni kuruhusu mmoja wa manaibu kuwa kaimu hata kwa mwezi mmoja, kisha ndani ya miezi mitatu tuitishe Mkutano Maalum wa Kitaifa wa Wajumbe (NDC) na kufanya mambo kwa njia sahihi,” alisema Bw Sifuna.
Bw Sifuna pia alihoji chanzo cha fedha ambazo ODM inatumia kuendesha mikutano ya Linda Ground.
“Fedha mnazoona zikitumika kwenye mikutano ya ODM hazitoki makao makuu ya ODM; kuna ufadhili wa kando kwa shughuli zinazovaa rangi za ODM,” alisema, akikanusha madai kuwa chama kinagharamia hafla hizo.
“Achana na mnachosikia watu wakisema. Timothy Bosire, Mweka Hazina, pia ni mtia saini wa akaunti za benki, na fedha za mwisho tulizotumia rasmi kama ODM zilikuwa za sherehe za Mombasa, nazo zilikuwa sehemu ndogo sana ya kile tulichoona huko,” aliongeza.
Akionekana kuwa mmoja wa viongozi wenye sauti kali ndani ya chama, Bw Sifuna amechukua misimamo ambayo wakati mwingine imekinzana na Bw Sifuna, kwa mfano, amesema chama kinapaswa kusimamisha mgombea wa urais mwaka 2027 na kisiunge mkono Dkt Ruto, kama inavyopendekezwa na sehemu ya uongozi wa ODM.
Alisema wale ambao hawako tayari kubeba bendera ya ODM kama wagombea wa urais wanapaswa kupisha walio tayari.