Makala

Huyu hapa Padri anayefuga mamba, kobe na nyani Nandi

Na MACHARIA MBUGUA February 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

PADRI wa Kanisa la Anglikana, Japhet Sugut ambaye pia ni Askofu Msaidizi alipoamua kufuga mamba katika shamba lake kaunti ya Nandi mwaka 2018, majirani wake katika kijiji cha Chepsangor walidhani amepotoka akili.
Hata hivyo, miaka mitano baadaye, hifadhi yake ya wanyamapori iliyojificha katika milima ya Nandi imekua na kuwa mradi unaostawi, unaovutia wanafunzi, watafiti na wageni wengine kutoka maeneo mbalimbali.
Kilichoanza kama jaribio dogo lakini la ujasiri katika uhifadhi wa wanyamapori, sasa kimekua na kuwa hifadhi iliyoidhinishwa rasmi, chini ya mpango wa Shirika la Huduma za Wanyamapori Kenya (KWS), unaoruhusu watu binafsi kuasili na kufuga wanyamapori kwa kuzingatia masharti madhubuti.
“Nilitaka kuunda fursa kwa wanafunzi kujifunza, wakazi kuona wanyamapori, na kuchangia katika uhifadhi wao,” alisema.
Kwa sasa, hifadhi hiyo ina mamba watatu waliokomaa, kobe na nyani wanaoishi kwa amani pamoja. Kuna mipango ya kuanzisha aina nyingine za wanyamapori siku zijazo. Ni mandhari adimu ambayo imegeuza shamba la kifamilia kuwa mojawapo ya vivutio vya kipekee zaidi katika Kaunti ya Nandi.
Hifadhi hiyo pia hutumika kama eneo la kiroho, ikiandaa shughuli za kidini kama Njia ya Msalaba chini ya kivuli cha miti asili. Askofu Sugut ameipa jina Bustani la Edeni.
Ili kuanzisha mradi huo, kasisi huyo alipata kibali cha kubadilisha matumizi ya ardhi kutoka kwa serikali ya kaunti, akibadilisha sehemu ya shamba lake kwa matumizi ya burudani na kidini.
KWS baadaye ilifanya tathmini ya eneo hilo, na baada ya kubaini mazingira yalikuwa salama kwa wanyama, ikampa leseni ya kufuga aina nne za wanyama na ndege.
Kati ya chaguo alizopewa na KWS, aliamua kufuga mamba, akisema alichagua wanyama adimu na wa kipekee katika eneo hilo.
Kwa mkewe, Bi Esther Sugut, wazo hilo lilikuwa la kutisha alipoelezwa kwa mara ya kwanza. Hakuwahi kufikiria kuishi karibu na wanyama hatari ambao taya zao zinaweza kumvunja mbuzi kwa sekunde chache.
“Aliponiambia mara ya kwanza, nilihisi hofu sana. Nikikua, nilijua mamba wanapaswa kuishi porini, si karibu na watu,” alikumbuka.
Hata hivyo, baada ya kuhakikishiwa kuhusu hatua za usalama na kuvutiwa na mazingira ya asili yanayozunguka shamba lao, polepole alikubali wazo hilo. Leo, anachangia katika jukumu muhimu la kulea wanyama hao kila siku.
Yeye ndiye mlezi mkuu wa hifadhi hiyo. Huwalisha mamba, husafisha mabwawa na hutembea miongoni mwao kwa ujasiri wa tahadhari—lakini tu wakiwa wameshiba, anasisitiza.
Kwa muda, anasema mamba hao wamezoea harufu na sauti yake, jambo linalomwezesha kuzunguka kwa usalama ndani ya eneo lao.
“Wanaitambua sauti yangu. Nikisema ‘croco, croco’, wanainua vichwa vyao. Wanajua kitu kizuri kinakuja,” alisema.
Mamba hulishwa sungura na kuku, kila mmoja akila angalau kilo moja na nusu ya nyama mara moja kila baada ya wiki tatu au nne.
Kwa wakazi wa kijiji, wazo hilo lilikuwa la kushangaza na lilizua hofu mwanzoni. Wengi walijiuliza kwa nini kasisi angefuga wanyama hatari katika eneo linalojulikana kwa mashamba ya chai, mahindi na ufugaji wa ng’ombe wa maziwa.
Bw Macurin Tirien, mkazi wa eneo hilo, anakumbuka alivyotahadhari na mabwawa hayo kwa hofu ya mamba kutoroka.
“Awali tulikuwa na wasiwasi mkubwa. Hata tulipoalikwa kuwaona, tulitazama kwa mbali. Hakuna aliyethubutu kukaribia,” alisema.