#KOMBOA Kenya: Kalonzo azindua jukwa la kuendesha kampeni ya kumng’oa Ruto 2027
KIONGOZI wa Wiper Patriotic Front, Kalonzo Musyoka, wikendi alizindua rasmi jukwaa la kuendesha kampeni zake za urais, akiahidi kubadilisha maisha ya Wakenya dhidi ya kile alichokitaja kuwa ni uongozi mbaya, ufisadi na kupanda kwa gharama ya maisha.
Uzinduzi huo ulifanyika miezi kadhaa baada ya Wiper kumuidhinisha rasmi Bw Musyoka kuwa mgombea wake wa urais.
Kuidhinishwa huko kulichukuliwa na washirika wake kama mwanzo wa kampeni zake za kuingia ikulu 2027.
Bw Musyoka atakuwa akiwania urais kwa mara ya pili baada ya kugombea mnamo 2007 na kumaliza nyuma ya marehemu Mwai Kibaki na Raila Odinga.
Bw Musyoka, katika mahojiano ya awali amewahi kusema kuwa kujiondoa tena katika kinyangányiro cha urais mnamo 2027 kungekuwa sawa na kustaafu siasa za ushindani.
Atakuwa akitumia kaulimbiu ya “Kalonzo 2027”.
Kwa mujibu wa kura ya maoni ya TIFA iliyotolewa mwezi uliopita, Bw Musyoka ndiye anayeshika nafasi ya pili kwa umaarufu miongoni mwa wanaotajwa kuwa wagombea wa urais.
Asilimia 19 ya Wakenya walimtaja kama chaguo lao kuu la urais.
William Ruto aliongoza kwa asilimia 24 huku Fred Matiang’i akifuatia kwa asilimia 14.
Akihutubia wafuasi, magavana, wabunge, wanadiplomasia, viongozi wa biashara na wanachama wa upinzani jijini Nairobi, Bw Musyoka alisema jukwaa hilo ni zaidi ya tovuti ya kampeni, akilitaja kama uzinduzi rasmi wa vuguvugu lake la “KOMBOA Kenya”.
Alisema vuguvugu hilo linalenga kuikomboa nchi kutoka kwa uongozi mbaya na kurejesha imani ya wananchi kwa viongozi wao.
“Huu si uzinduzi wa tovuti pekee. Huu ni wakati wetu wa KOMBOA,” akasema.
Bw Musyoka alisema Kenya imefika katika njia panda, akitaja ongezeko la ushuru, kupungua kwa mapato, ukosefu wa ajira, deni la umma linaloongezeka na kutoridhika kwa wananchi kuhusu utawala wa Rais Ruto.
“Tumeshuhudia mamlaka bila misingi. Tumeona mvuto wa kisiasa bila maadili. Tumeishi katika enzi ya ahadi zinazotekelezwa kabla hata wino wa kiapo haujakauka,” akaongeza.
“KOMBOA Kenya si kampeni inayofadhiliwa na makundi ya kifisadi au kuendelezwa na ufisadi. Hili ni vuguvugu la wananchi, na wananchi ndio wanapaswa kulipa nguvu,” akasema.
Gavana wa Machakos, Wavinya Ndeti, alifananisha kampeni hiyo na ile ya Rais wa zamani wa Amerika Barack Obama na kuwahimiza Wakenya kuunga mkono azma ya Bw Musyoka kupitia michango ya kifedha.
“Tunawaomba Wakenya wenye nia njema kumuunga mkono. Tunataka Wakenya wamiliki ugombea huu wa urais, si mafisadi na madalali wa kisiasa,” akasema Bi Ndeti.
Gavana wa Kitui County, Julius Malombe, alisema uzinduzi huo unaashiria mwanzo rasmi wa kampeni za urais za Bw Musyoka na kuthibitisha tena uungwaji mkono wa Wiper kwa ugombea wake.
“Hili ni jukwaa linalowajumuisha wote, na kama Wiper tumemteua kuwa mgombea wetu wa urais. Amehudumu serikalini kwa muda mrefu, ni mtu mtulivu na mwenye busara ambaye ataiongoza nchi hii kwa umakini unaostahili,” akasema Bw Malombe.