Makala

Kenya kuanza kuchuma mapato kutokana na mauzo ya mafuta ghafi kutoka Turkana-Wandayi

Na WINNIE ONYANDO June 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KENYA itaanza kuzalisha mafuta kabla ya mwisho wa mwaka huu kutoka kaunti ya Turkana kaskazini mwa nchi.

Waziri wa Kawi na Mafuta Opiyo Wandayi hivyo Ijumaa Juni 5, 2026 alifafanua kuwa ni mafuta ghafi yatakayozalishwa na kuuzwa ng’ambo kusafishwa kutoa petroli, dizeli na bidhaa nyinginezo.

“Kabla ya mwisho wa mwaka huu tutaanza kuzalisha mafuta kutoka Turkana. Baada ya muda mrefu hatimaye utekelezaji wa mradi huu umepiga hatua hadi kufikia kiwango cha uzalishaji,” akaeleza kwenye mahojiano katika Radio Jambo, akiutaja mradi huo kama yenye umuhimu mkubwa katika sekta ya kawi.

“Mafuta ghafi kutoka Turkana yatauzwa ng’ambo kwa sababu wakati huu hatuma kiwanda cha kusafisha mafuta. Mapato kutkana na uuzaji wa mafuta hayo yatafaidi Wakenya wote sio tu wakazi wa Turkana,” Bw Wandayi akaeleza.

Mwezi jana, Rais William Ruto alifichua mpango wa kuanzishwa kwa kiwanda cha kusafisha mafuta katika ukanda wa Afrika Mashariki, kwa ushirikiano na bwanyenye wa Nigeria Aliko Dangote.

Alisema kuwa kampuni hiyo itaanzishwa eneo la Tanga, nchini Tanzania.

Kampuni ya Gulf Energy Ltd ndio itakuwa ikichimba mafuta kutoka visima vilivyoko Lokichar, eneo bunge la Turkana Kusini.

Kampuni hiyo ilitwaa usimamizi wa mradi huo baada ya kutwaa shughuli ya mali ya kampuni ya Tullow Oil, ya Uingereza, iliyoanzisha uchimbaji wa mafuta eneo hilo miaka 10 iliyopita.

Wakati huu Kenya hununua mafuta yaliyosafishwa kutoka ukanda wa Mashariki ya Kati, linaloshuhudia vita kati ya Amerika na Iran.

Vita hivyo vilivyoanza Februari 28, vimevuruga usafirishaji wa bidhaa hiyo kupitia Mkondo wa Hormuz, hali ambayo imechangia kupanda kwa bei ya mafuta nchini.

Hata hivyo, mapema wiki huu Waziri Wandayi alielezea matumaini  kuwa bei ya mafuta itashuka hivi karibuni, baada ya serikali kuanza kupata mafuta kwingineko, hali itakayoleta afueni kwa Wakenya