Azimio ni marehemu bila ODM, adai Ruto akimpiga Uhuru kijembe
RAIS William Ruto amesema mabadiliko ya uongozi yaliyofanyika katika muungano wa Azimio la Umoja hayana mashiko, akisema muungano huo ni ‘mfu’ bila ODM.
Akizungumza mtaani Pipeline, Embakasi Kusini jana baada ya kuhudhuria ibada eneo hilo, Rais alisema mabadiliko hayo yaliyotekelezwa na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta hayana uzito wowote kisiasa.
Kulingana na Rais, ODM ambayo ilikuwa mhimili katika muungano huo kwa sasa iko katika Serikali Jumuishi na inashirikiana na utawala wa Kenya Kwanza.
“Nimesikia kuwa sasa wanafufua Azimio, ile tulishinda asubuhi na mapema. Azimio bila ODM ilishazimia,” akasema Rais Ruto.
Aliwataka wajiepushe na ‘hadaa’ za kisiasa za wapinzani wake na wamuunge mkono mnamo 2027.
Kauli yake inajiri baada ya mkutano wa wiki jana ulioandaliwa na Bw Kenyatta ambapo Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka aliteuliwa kiongozi mpya wa muungano huo huku Caroli Omondi akipata wadhifa wa katibu mpya.
Bw Musyoka alichukua wadhifa huo kutoka kwa marehemu Raila Odinga ambaye alikuwa mwaniaji wa urais wa muungano huo 2022 huku Bw Musyoka akiwa mgombeaji mwenza.
Katika mabadiliko hayo Katibu wa zamani wa Jiji Kuu Philip Kisia aliteuliwa Mkurugenzi Mkuu huku Mbunge wa Suna Mashariki Junet Mohamed akiondolewa kama katibu mkuu wa Azimio.
Kauli ya Rais inatokea wakati ambapo uongozi wa ODM umepinga mabadiliko hayo na kuiandikia barua Afisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP).
Wakati wa ziara yake Embakasi, Rais pia alizungumzia mafanikio ya utawala wake Nairobi na sehemu nyingine za nchi.
Alisema kuwa ataendelea kushirikiana na upinzani kuhakikisha jiji la Nairobi ni safi na lina mwangaza.
“Nairobi ndiko mabadiliko ya nchi yataanzia kwa sababu hatuwezi kubadilisha nchi kama Nairobi haijabadilishwa,” akasema Kiongozi wa nchi.
Alisema wanajenga nyumba 169,000 za gharama nafuu kwa wakazi wa Nairobi akiahidi kuwa kila mkazi lazima awe na makazi mazuri.
“Nataka niwaambie kuwa baada ya miaka 15 hakutakuwa na mitaa ya mabanda hapa Nairobi. Hatuwezi kuwa na jiji kuu ambalo watu wanaishi mitaa ya mabanda,” akasema.
Aliahidi kuwa uzoaji taka utaendelea Nairobi na mnamo Aprili serikali ya kaunti na ile ya kitaifa zitashirikiana kwenye mpango wa uzoaji taka.
Rais alikuwa ameandamana na Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja, Naibu Gavana James Muchiri na madiwani kutoka Bunge la Kaunti ya Nairobi.