Habari za Kaunti

Wakazi waanza kuvuna shughuli zikiongezeka bandarini Lamu, Dangote akikaribia kuja

Na ANTHONY KITIMO August 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAKAZI wa Kaunti ya Lamu wana sababu ya kutabasamu huku Bandari ya Lamu ikiendelea kuvutia meli nyingi zaidi, hali inayotarajiwa kuleta nafasi za ajira na kukuza biashara katika eneo hilo.

Mamlaka ya Bandari Kenya (KPA) imesema bandari hiyo imepokea meli 167 tangu Januari mwaka huu na idadi hiyo inatarajiwa kufikia karibu meli 200 kufikia Septemba.

Mwaka jana, bandari hiyo ilikuwa imehudumia chini ya meli 50 katika kipindi kama hicho.

Ongezeko hilo limechangiwa na mabadiliko ya njia za usafirishaji wa baharini kufuatia mvutano wa Mashariki ya Kati, ambapo baadhi ya kampuni za usafirishaji zimehamishia shughuli zao Lamu.

Wafanyakazi wakiendelea na shughuli za ujenzi katika bandari ya Lamu katika picha hii ya Agosti 27, 2019. Picha|Maktaba

Kwa wakazi wa Lamu, ongezeko la shughuli bandarini linamaanisha ajira zaidi kwa madereva, wapakiaji, mawakala wa forodha, wafanyabiashara wa chakulana wamiliki wa nyumba za kupanga na watoa huduma mbalimbali.

Meneja Mkuu wa Bandari ya Lamu Abdulaziz Mzee, alisema mwaka 2026 unaonekana kuwa bora zaidi tangu bandari hiyo izinduliwe mwaka wa 2021.

“Tunaendelea kushuhudia ongezeko la meli zinazoingia bandarini. Pia tunawekeza katika korongo mpya za kupakia na kupakua mizigo pamoja na vifaa vingine ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka,” alisema.

Aidha, maelfu ya magari yaliyogeuzwa kutoka Bandari ya Dubai kuelekea Lamu yameongeza shughuli za usafirishaji na kuhifadhi mizigo, hatua iliyowanufaisha wafanyabiashara wa eneo hilo.

Wataalamu wa uchukuzi wa baharini wanasema ikiwa Serikali itaharakisha ujenzi wa barabara na miundombinu ya mradi wa LAPSSET, Bandari ya Lamu itakuwa kitovu kikuu cha biashara Afrika Mashariki na kufungua fursa zaidi za ajira na maendeleo kwa wakazi wa eneo hilo.