Waasi wa ODM sasa wafyatuka, waanza kujipanga
JOTO la kisiasa linaendelea kutokota ndani ya ODM baada ya viongozi waasi katika chama hicho kusema kuwa watapambana hadi mwisho kuzui chama ‘kuuziwa’ Rais William Ruto.
Wanasiasa hao ambao wanapinga Serikali Jumuishi jana walianzisha misururu ya mikutano wakianza na kaunti za Busia na Siaya ambapo waliapa kuwa watalinda falsafa ya uongozi wa marehemu Raila Odinga ambaye alikuwa kiongozi wa chama hicho kabla ya kuaga dunia Oktoba 15.
Aidha, walisimama kidete na kusema hakuna mwenye mamlaka ya kuwafukuza katika ODM, wakiahidi kuendeleza mtindo wa chama hicho wa kupigania haki ya mwananchi wa kawaida.
“Rais hajaheshimu ajenda 10 ambazo Raila alituachia. Kama alimkaidi Raila, unafikiri sasa ataheshimu makubaliano ya kisiasa na Dkt Oburu Oginga?” akauliza Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna katika uwanja wa Busia, mkutano ambao ulihudhuriwa na halaiki ya watu.
Bw Sifuna aliandamana na Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, Seneta wa Kisii Richard Onyonka, mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Caleb Amisi (Saboti), Anthony Kibangendi (Kitutu Chache Kusini) na Katibu Mkuu wa Azimio la Umoja-One Kenya Caroli Omondi (mbunge wa Suba Kusini).
Wengine waliokuwepo ni Mbunge wa Wiper anayewakilisha Kaiti Joshua Kimilu, Obadia Barongo wa Bomachoge na mwanaharakati Brian Weke.
Kila kiongozi aliyehutubu alishutumu mazungumzo yanayoendelea kati ya Rais Ruto na Dkt Oginga, wakisema watatumia mikutano maarufu kama ‘Linda Mwananchi’ kuzuia chama hicho cha Chungwa kunadiwa kwa serikali.
Bw Sifuna alisema viongozi waliokuwa Busia ndio majemedari halisi wa marehemu Raila wala hawataruhusu chama kichukuliwe na mtu mwingine wa nje.
“Wanatuita waasi tukiyauliza maswali muhimu yanayohusu raia lakini hatutaogopa. Raila hakuwalea muwe waoga,” akaongeza Bw Sifuna.
Seneta huyo alisema makataa ya kutekeleza ajenda 10 na serikali ni Machi 7 wala muda huo hautarefushwa. Alisema ni Raila pekee ndiye anayeweza kusongesha muda huo kupitia saini yake.
Gavana Orengo naye alishutumu kundi linaloegemea mrengo wa Dkt Oginga kwa kupanga kuuza chama na kusema hawataruhusu hilo.
Bw Orengo aliapa kuwa hata watishwe kwa njia gani, wataendelea kuzungumzia maovu ya utawala wa Rais Ruto.
“Hatuwataki watu wanaoangalia matumbo yao ndani ya ODM. Hakuna mtu atakayeuza ODM wala haitamezwa na chama chochote kwa sababu kila kitu ODM inafanya kinahusu maslahi ya raia,” akasema Bw Orengo.
Gavana huyo alisema nia ya baadhi ya viongozi ni kunufaika kwa uteuzi serikalini badala ya kuzingatia maono ya ODM.
“Hata Raila alituambia tusiangalie tu vyeo ila maslahi ya wananchi. Hivi karibuni wanaojaribu kuuza ODM hawatakaribishwa hapa Busia, ODM inaweza kuwa na mwaniaji kwa sababu tuna viongozi ambao wamehitimu,” akaongeza Bw Orengo.
Bw Osotsi ambaye ni naibu kiongozi wa ODM alisema hawataruhusu Rais atumie ‘mlango wa nyuma’ kudhibiti chama chao akiwataka wote wanaopinga serikali waongee bila hofu.
“Tuna viongozi wanaotosha kuwania urais wala hatufai kutishwa. Tunatishiwa lakini nawaambia wenzangu wasiingiwe na hofu wala uoga,” akasema Bw Osotsi.
Alishutumu serikali kwa kushindwa kuwalipa fidia wahanga wa maandamano jinsi ilivyoahidi Raila alipokuwa hai.
Bw Babu Owino naye alimshutumu Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi akisema hakuna haja ya viongozi kudai Luo Nyanza iko serikalini ilhali hainufaiki na utawala wa sasa.
“Baadhi ya viongozi wanaangalia tu matumbo yao kwa sababu huwezi kuimba ‘tutam’ ilhali vijana hawana kazi, sekta ya elimu ipo pabaya na wahanga wa maandamano hawajalipwa,” akasema Bw Owino.
“Mnamo 2027 tutakuwa na mageuzi ambayo yatawapa vijana kazi. Wanatuambia tusiandae maandamano ilhali ndiyo yaliwapa Wandayi na John Mbadi kazi serikalini,” akaongeza.
Mjini Ugunja, kundi la umati lilizomea viongozi hao na kuwaimbia ‘Tutam’ lakini wakaendelea na hotuba zao bila kutetereka.
Baada ya hapo walifululiza hadi Sega, Bumala na kuandaa mkutano mkubwa wa kisiasa uwanja wa Busia.
Awali Mbunge wa Alego Usonga Sam Atandi aliandaa mkutano mjini Siaya na kuwataka wananchi wasiruhusu kundi la Bw Orengo mjini humo.