MAONI: KICD ilikosea kutenganisha lugha na fasihi ya Kiswahili
MUSTAKABALI wa somo la fasihi ya Kiswahili katika mifumo ya elimu nchini Kenya haujulikani, baada ya kubainika kwamba, somo hilo linateuliwa na wanafunzi wachache mno.
Wakati huo huo, wataalamu wa Kiswahili wameonya kwamba, pana hatari ya kukosa wanafunzi watakaosomea somo hilo katika vyuo vikuu, baada ya Taasisi ya Ukuzaji wa Mitaala ya Kenya (KICD) kutenganisha masomo ya lugha na fasihi, kwenye Mtaala mpya wa Elimu ya Kiumilisi (Competency Based Education).
Hatua ya kutenganisha masomo ya lugha na fasihi na kuyafanya huru katika kiwango hicho huenda yalinuia kupanua mawanda ya ufunzaji wa fasihi – lakini kuna dalili za wazi kwamba, kufanya hivyo ni ‘kosa kubwa’ linalopaswa kurekebishwa mara moja – la sivyo litaangamiza kizazi kizima ‘kinachokwepa’ kuteua fasihi na kukimbilia masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati – maarufu kama STEM.
Akichangia mdahalo unaoendelea nchini kuhusu ‘kosa’ hilo, mtaalamu wa fasihi katika Chuo Kikuu cha Nairobi, Prof Mwenda Mbatiah aliuliza: Je, uamuzi wa kutenganisha lugha na fasihi ulifikiwaje? Ulihusiana na walimu kuchukia au kutoona umuhimu wa fasihi?”
Wakuza Mitaala wa KICD huenda walitenganisha masomo ya fasihi na lugha kwa ‘nia njema’ – kulifanya somo la Fasihi ya Kiswahili kuwa somo kamili.
Dhamira hiyo labda ilikuwa ni kuwapatia fursa wanafunzi wa Gredi ya 10 hadi 12 kujifunza fasihi simulizi, bunilizi na kazi za kihalisia.
Ikiwa lengo lilikuwa ni hilo, huenda lisitimie, baada ya wanafunzi waliojiunga na Gredi ya 10 ‘kususia’ au kukataa kuteua somo la fasihi.
Prof Mbatiah anasisitiza kwamba, somo la fasihi kote ulimwenguni ni kiungo muhimu katika kukuza na kumjenga mtu na ubinadamu wake: “Inafaa kukumbushana faida za wanafunzi kusoma lugha na fasihi pamoja. Kwanza, taaluma kama uanahabari, (utangazaji na uandishi) hutegemea sana mbinu za kifasihi. Pili, tunahitaji wasanii: Waimbaji, waigizaji. Mwisho, fasihi ni nyenzo kuu ya kufunzia na kukongomelea maadili kama utu na uzalendo,” anashauri Prof Mbatiah.
Katika shule moja, Kaunti ya Tharaka Nithi (jina limebanwa), kwa mfano, kati ya wanafunzi 775 waliojiunga na gredi ya 10, ni wanne (4) tu walioteua somo la fasihi.
Hali hiyo imebainika kote nchini. Barua kwa maafisa wa elimu katika kiwango cha kaunti, kutoka kwa Katibu katika Wizara ya Elimu, Prof Julius Bitok iliyoandikwa Agosti 8, 2025, inashauri kuwa, wanafunzi wanaojiunga na Shule Pevu wanapaswa kusoma Masomo Saba (7) ilivyopendekezwa na Jopokazi la Rais kuhusu Marekebisho ya Mfumo wa Elimu (PWPER, 2023).
KICD inapaswa kuchukua hatua za dharura kurekebisha mtaala wa Kiswahili.
Bitugi Matundura ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Chuka