Mwalimu anayebadilisha mtazamo wa wanafunzi wasiopenda Ushairi na Sarufi
KATIKA kipindi ambapo jamii nyingi zinakabiliwa na changamoto za malezi, nidhamu na maadili, bado wapo walimu wanaosimama imara kama nguzo za matumaini.
Wao hawafundishi darasani pekee, bali huishi maisha yanayowapa wanafunzi mfano wa kuigwa. Kupitia juhudi zao, wanafunzi wengi hupata mwelekeo sahihi na kuhamasika kufikia ndoto zao.
Miongoni mwa walimu hao ni Bi Valentine Nayaku, mwalimu wa Kiswahili katika Shule ya Upili ya Itabua, Kaunti ya Embu.
Safari yake ya mafanikio ni ushahidi kwamba bidii, nidhamu na uongozi bora vinaweza kumwezesha mtu kufikia kilele cha ufanisi.
Nayaku alizaliwa na kulelewa katika eneo la Malava, Kaunti ya Kakamega.
Yeye ndiye mwanambee katika familia ya watoto wanane ya Bw Antony Inyanje na Bi Linet Lelei. Tangu akiwa mtoto, alionyesha ari kubwa ya kujifunza na kujituma katika masomo yake.
Safari yake ya elimu ilianzia katika Shule ya Msingi ya Lugusi kabla ya kupitia katika Shule ya Upili ya Kongoni.
Akiwa mwanafunzi, alivutiwa sana na uigizaji pamoja na ughani wa mashairi aliyoyasikia redioni na runingani. Hata hivyo, mapenzi yake makubwa yalikuwa kwa somo la Kiswahili.
“Walimu wangu kama Bw Lumasai, Edward Barasa, Seth Ambei na Makhanu walinilea na kuninoa katika Kiswahili. Aidha, walimu wangu wa darasa, Bw Kelvin Mutali na Bw Daniel Wemanya, walinishauri nichague taaluma ya ualimu wa Kiswahili ili niendelee kung’ara katika lugha hii,” anasimulia.
Uongozi wake ulianza kujidhihirisha akiwa shuleni alipoteuliwa kuwa kiranja tangu kidato cha pili.
Nafasi hiyo ilimjenga kuwa kiongozi mwajibikaji mwenye nidhamu ya hali ya juu.
Walimu wake, akiwemo Bw Nyabera na Bi Sheila Sifuna, walimpa mwongozo ulioimarisha uwezo wake wa kuongoza hadi alipokamilisha masomo ya shule ya sekondari.
Baada ya kuhitimu, alijiunga na Chuo Kikuu cha Embu kusomea shahada ya ualimu (Kiswahili/Historia).
Huko, hakujitokeza tu kuwa mwanafunzi mahiri, bali pia kiongozi mashuhuri.
Alichaguliwa kuwa mwakilishi wa wanafunzi wa Kiswahili kwa miaka minne na akawa mwanachama hai wa Chama cha Kiswahili cha Embu (CHAKIE).
Uwezo wake wa uongozi ulimwezesha kupanda ngazi kutoka Katibu Mkuu hadi Mwenyekiti wa chama hicho.
Umahiri wake ulivuka mipaka ya chuo na kumfikisha katika Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili katika Vyuo Vikuu vya Afrika Mashariki (CHAWAKAMA–KENYA), ambapo alihudumu akiwa Katibu Mtendaji na baadaye Afisa wa Nidhamu.
Bi Nayaku anawashukuru sana Dkt Timothy Kinoti na Dkt Wanyama kwa mchango wao mkubwa katika kumkuza kitaaluma hadi alipohitimu mwaka wa 2023.
Pia anawakumbuka Bw Oscar na Bi Florence, viongozi wa dini waliomkaribisha na kumwelekeza vyema alipokuwa chuoni.
Baada ya kuhitimu, alifundisha katika Shule ya Upili ya Kongoni kwa miaka miwili kabla ya kuhamia Shule ya Upili ya Itabua.
Leo, anaendelea kutekeleza ndoto yake ya kutumia Kiswahili kubadilisha maisha ya wanafunzi.
“Nilitamani kuwa mwalimu wa Kiswahili ili nibadilishe mtazamo wa wanafunzi wasiopenda ushairi na sarufi, kisha niwasaidie kuwa wataalamu na viongozi bora wa baadaye,” anasema kwa tabasamu.
Kupitia moyo wake wa kujitolea, mapenzi kwa Kiswahili na uongozi wa kuigwa, Bi Nayaku anaendelea kuwasha taa ya matumaini kwa kizazi cha sasa na kijacho.