Mali ya binti ya Michuki hatarini kupigwa mnada katika mzozo wa madeni
MKONO wa sheria umeibua kile kilichokuwa kimefichika, baada ya mahakama kuamua kuwa aliyekuwa mwanachama wa Bodi ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Kenya (KAA), Bootsy Mutiso, pamoja na Sheila Murugi, binti wa aliyekuwa waziri marehemu John Michuki, lazima walipe madeni waliyokubali kusuluhisha kabla ya kuuza kampuni ya Flex Air Charters Ltd.
Bw Mutiso na Bi Murugi sasa wanakabiliwa na hatari ya mali yao kuuzwa kwa mnada, huku wenyehisa wapya wa Flex Air Charters wakitaka kurejeshewa fedha walizolazimika kulipa kwa mkopeshaji ambaye tayari alikuwa ameshinda kesi dhidi ya kampuni hiyo ya shughuli za angani.
Uamuzi huo wa Mahakama ya Hakimu Mkuu katika Mahakama za Milimani, Nairobi, unaweza kuwalinda wawekezaji dhidi ya madai ya madeni yaliyokuwepo kabla ya ununuzi wa kampuni, pale ambapo wenyehisa wa awali walikubali kubeba mzigo wa madeni baada ya kuuza hisa zao na kuacha udhibiti.
Bw Mutiso na Bi Murugi walimiliki pamoja Flex Air Charters kabla ya kuuza hisa zao kwa Namanga Aviation Ltd mnamo Julai 20, 2020.
Ingawa mabadiliko ya umiliki yalitarajiwa kurekodiwa rasmi na Msajili wa Kampuni, makubaliano ya ununuzi wa hisa yalijumuisha mkataba wa faragha uliowafanya wawili hao kuwa “wadaiwa wasioonekana”.
Kifungu katika mkataba huo kilieleza kuwa Bw Mutiso na Bi Murugi wangewajibika kulipa madeni yote yaliyokuwepo kabla ya mabadiliko ya umiliki ya Julai 2020.
Stakabadhi za mahakama zinaonyesha kuwa Namanga Aviation Ltd, mmiliki wa sasa wa Flex Air Charters, inamilikiwa na Esther Njoroge na Nicholas Njoroge.
Miaka mitatu baada ya mauzo ya hisa kukamilika, kampuni ya kukodisha helikopta ya Lady Lori iliwasilisha madai dhidi ya Flex Air Charters ikitaka kulipwa dola 39,794 (takriban Sh5.13 milioni), deni lililolimbikizana kati ya Novemba 2018 na Januari 2020.
Deni hilo lilitokana na Flex Air Charters kukodisha helikopta kutoka Lady Lori.
Flex Air Charters ilipowataka Bw Mutiso na Bi Murugi walipe deni hilo, wawili hao walikana kuwajibika.
Msimamo huo uliwaacha wenyehisa wapya wa Flex Air Charters wakikabiliwa si na deni tu la Lady Lori, bali pia madai ya wadai wengine waliokuwa na madeni ya kabla ya Julai 2020.
Kabla ya mabadiliko ya umiliki, Flex Air Charters ilikuwa inadaiwa na wadai 10 jumla ya dola 99,387 (takriban Sh12.82 milioni).
Mwaka 2023, Lady Lori iliishtaki Flex Air Charters ikitaka Sh5.1 milioni pamoja na riba na gharama za kesi.
Flex Air Charters nayo iliwasilisha kesi dhidi ya Bw Mutiso na Bi Murugi, ikiomba mahakama iamuru wawili hao walipe Sh5.1 milioni.
Hakuna kati ya wawili hao aliyewasilisha majibu mahakamani. Mahakama ya Hakimu Mkuu ilikubali ombi la Flex Air Charters na kutoa uamuzi wa haraka dhidi ya Bw Mutiso na Bi Murugi.
Waliamriwa kulipa Sh6.43 milioni ili kurejesha fedha ambazo wanahisa wapya walilazimika kulipa Lady Lori.
Uamuzi huo umefungua njia kwa Flex Air Charters kufuatilia mali za Bw Mutiso na Bi Murugi kwa lengo la kuiuza kwa mnada ili kurejesha deni.
Aidha, umeweka msingi wa kisheria kwa madeni mengine ya awali ya Flex Air Charters kabla ya kununuliwa na Namanga Aviation.
Uamuzi wa mahakama unaashiria kuwa hata kama wanahisa wapya wa Flex Air Charters watalazimika kulipa madeni hayo ya kihistoria, wana uwezekano mkubwa wa kupewa amri za kuwafuatilia Bw Mutiso na Bi Murugi ili kurejeshewa fedha hizo.