Majangili wavamia kijiji kinachohifadhi wahanga wa ukame na kuiba mifugo mchana
KIJIJI cha Lokwamosing kaunti ya Turkana Mashariki, ambacho kwa muda mrefu kimekuwa kimbilio la wafugaji wanaokabiliwa na ukame mkali, kiligeuka uwanja wa maafa Jumatatu baada ya zaidi ya majangili 200 wenye silaha malisho ya kijamii na kuiba maelfu ya mifugo.
Lokwamosing kinajulikana kwa chemchemi ya kudumu na nyanda zenye malisho laini.
Eneo hilo limekuwa tegemeo la mamia ya mifugo kutoka maeneo yaliyokumbwa na ukame mkali huku malisho yakizidi kupungua.
Hata hivyo, majira ya saa tatu asubuhi Jumatatu, majangili hao walivamia kijiji hicho na kuondoka n zaidi ya mifugo 2,000 mchana peupe.
Washambuliaji waliwazidi nguvu polisi wa akiba watano waliokuwapo, huku wachungaji wengi wakiwa vijana wasio na silaha.
Malisho hayo hutumiwa na wafugaji kutoka vijiji vya Lopii, Kaakulit, Lochakula, Nakwakaal, Kahuruko na Arumrum Alokaaran.
Stephen Ekadeli, mkazi wa Lokwamosing aliyepoteza mifugo wake wote, alisema: “Mifugo wasiporejeshwa nitapata fedheha kubwa kama mfugaji wa Turkana.
Nilikuwa na ngamia na ng’ombe. Sasa nalala nikiwa maskini kiuchumi na kitamaduni.”
Majangili waliendesha mifugo kuelekea Lochakula, makazi ya zamani ya Waturkana ambayo sasa yanadaiwa kukaliwa na wahalifu wenye silaha.
Wanakijiji waliarifu Kamati ya Usalama ya Kaunti Ndogo, na Gavana Jeremiah Lomorukai akafahamisha maafisa kutoka Lokori wakiwemo wa Kitengo cha Kupambana na Fujo (GSU) na Huduma ya Kitaifa ya Polisi.
Zaidi ya mbuzi 150 waliokolewa kabla ya msako kusitishwa kilomita 40 kutoka Lochakula.
Gavana alisema majangili walichoma vichaka kuficha nyayo zao kabla ya kutorokea mabonde ambayo ni vigumu ya kufika.
Alionya kuwa chemchemi ya kudumu ya Lokwamosing imekuwa kitovu cha mashambulizi kwa kuwa ndiyo chanzo pekee cha maji.
Zaidi ya mashambulizi matano yameripotiwa tangu Januari katika mpaka wa Turkana na Pokot Magharibi.
Shule ya Lokwamosing ECDE na Shule ya Msingi ya Lokwamosing zimefungwa kwa hofu ya usalama.
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, alipozuru Kainuk kufuatia shambulio jingine majuzi, alitangaza operesheni kali dhidi ya makundi yenye silaha, akiahidi kurejesha amani katika mpaka wa Turkana na Pokot Magharibi.