Afya na Jamii

Sababu za mbu kuongezeka na jinsi ya kuwazuia

Na HELLEN SHIKANDA February 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUENDA umegundua ongezeko la mbu hivi karibuni. Si wale wa kujificha tena. Hawajali unapojaribu kuwafukuza.

Wanatua sehemu moja ya mwili, ukiwapiga wanahama hadi nyingine. Wakikuuma wanaacha mwasho wa muda mrefu, na milio yao inakera hata mchana.

Lakini je, kweli kuna ongezeko la mbu? Dkt Eric Ochomo, mtaalamu wa wadudu katika Taasisi ya Utafiti wa Matibabu Kenya (KEMRI) anathibitisha kuwa kuna ongezeko la mbu nchini.

Wanasayansi wa Kemri hufanya ufuatiliaji wa mara kwa mara katika takriban maeneo 60 kote nchini.

Akizungumzia Nairobi, Dkt Ochomo anasema aina mbili kuu za mbu ndizo zinawasumbua wakazi kwa sasa, Aedes na Culex.
Kwa mujibu wa tafiti za sasa, aina hizi mbili jijini Nairobi hazijasambaza magonjwa yoyote.

Mbu aina ya Aedes huonekana zaidi mchana. Ni wakubwa kidogo, wenye rangi nyeusi na mistari mieupe, hivyo ni rahisi kuwaona.

Wakikuuma kuna maumivu, na hata baada ya kuuma hawaruki mbali.

“Ni mbu wavivu na wakaidi,” asema Dkt Ochomo akieleza kuwa huwa wanazaliana katika mapipa ya maji yaliyo wazi, tairi za zamani, vyombo vifupi vyenye maji na mifereji ya maji taka iliyo wazi.

Kwa upande mwingine, mbu wa Culex huwa na kelele na hutokea zaidi usiku. Pia ni wakubwa na rahisi kutambulika.

Mbu wanaosababisha malaria ambao bado hawajarekodiwa kwa wingi Nairobi, ni wadogo na wasiri zaidi.

Kwa nini idadi yao inaongezeka? Dkt Ochomo anasema joto la juu linaweza kuchangia, na mabadiliko ya tabianchi yanaweza kufanya hali kuwa mbaya zaidi.

“Mbu hustawi katika hali ya joto,” asema.

Hata hivyo, anasisitiza kuwa chanzo kikuu ni tatizo la usafi wa mazingira.

“Usipomwaga maji na yabaki katika hali ya joto, mbu hupata mazalia mazuri,” anaonya.

Mbu hukomaa kutoka yai hadi kuwa mbu mzima ndani ya siku saba tu. Jike hutaga hadi mayai 500 kwa mara moja. Joto likiwa juu, uzalishaji huongezeka haraka zaidi.

Kaunti zinahimizwa kushughulikia tatizo la maji taka na mifereji.

Maeneo ya ujenzi yenye mashimo ya maji yasiyodhibitiwa pia yanatajwa kuwa hatari.

Tatizo hili si la Nairobi pekee.

Turkana, ambako joto ni kali na visima vingi vinachimbwa, maji machafu yasiyodhibitiwa yamechangia kuongezeka kwa mbu, hali ambayo imeongeza visa vya malaria.

Dkt Ochomo anashauri wananchi kumwaga maji yaliyotuama kwenye vyombo, matairi na matangi yaliyo wazi ili kupunguza mbu kuzaana.

Utafiti uliochapishwa katika jarida la BMC mwaka jana pia unaonya kuwa ukuaji wa miji barani Afrika na mabadiliko ya tabianchi huenda ukaongeza zaidi idadi ya mbu aina ya Aedes siku zijazo.