Ni joto kali Kajiado Nkedianye na Lenku wakiwinda useneta baada ya kuwa magavana
GAVANA Joseph Lenku na mtangulizi wake David Nkedianye wanatarajiwa kukwaruzana tena, wawili hao wakisaka useneta mnamo 2027.
Katika chaguzi za 2017 na 2022, wawili hao walikuwa na uhasama mkali wa kisiasa, huku Bw Lenku akishinda ugavana mara mbili.
Mnamo 2017, Gavana Lenku alimshinda Bw Nkedianye ambaye alikuwa amehudumu kama mkuu wa kaunti hiyo kutoka 2013-2017 kupitia ODM. Mwaka huo Bw Lenku alipata ushindi kupitia chama cha Jubilee.
Kwenye kura ya 2022, wawili hao walifarakana huku Bw Lenku akiwika tena. Bw Nkedianye ambaye alikuwa ODM aligura chama hicho na kuingia Jubilee huku Gavana Lenku naye akigura Jubilee na kuingia ODM.
Awali kulikuwa na jitihada zilizoendelezwa za kuhakikisha wawili hao wanaelewana ili kuwe na mwaniaji mmoja wa ugavana chini ya Muungano wa Azimio.
Hata hivyo, wawili hao waliachwa wamenyane huku Bw Lenku akipata kura 117,600 naye Nkedianye akipata kura 75,337. Katoo Ole Metito ambaye aliwania kupitia UDA alipata kura 111,752.
Mnamo Juni 2, 2023, Rais William Ruto alimteua Bw Nkedianye kuwa Mwenyekiti wa Taasisi ya Utafiti na Mafunzo Kuhusu Wanyamapori kwa muda wa miaka mitatu. Hii ni baada ya Bw Nkedianye kuhamia UDA mnamo Septemba 12, 2023.
Bw Nkedianye kwa sasa anashirikishiana na Bw Ole Metito ambaye analenga ugavana tena 2027. Wameelewana kuwa Bw Nkedianye atawania useneta naye Bw Ole Metito ambaye anafanya kazi ikulu agombee ugavana.
Seneta wa sasa Samuel Seki ambaye alichaguliwa kupitia tiketi ya UDA amekuwa akihusishwa na DCP naye pia analenga ugavana.
Seneta Maalum Peris Tobiko na Naibu Gavana Martin Moshisho ambao wote wapo mrengo wa Bw Lenku nao pia wanalenga kiti cha ugavana.
Bw Lenku ametoa wito wa kubuniwa kwa Chama cha Kisiasa cha jamii ya Maa huku akisema anaunga kuchaguliwa kwa Rais Ruto muhula wa pili.
“Ruto amerejesha mbuga ya Amboseli kwa serikali ya kaunti na naamini njia ya kumlipa ni kumpigia kura tena. Raia hawatashawishiwa na vyama vya kisiasa bali utendakazi wa kila kiongozi,” akasema Bw Lenku.
Naye Bw Nkedianye amekuwa akisisitiza kuwa ndiye anatosha kuwania useneta naye pia akiunga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto.
“Tutazunguka mijini na mashinani ili kujaza kura za Rais Ruto. Pia naamini kuwa ushirikiano kati ya ODM na UDA utatumika kuamua mwaniaji na kuhakikisha kura zinaelekezwa kapu moja,” akasema Bw Nkedianye.