Wanachama wa UDA ‘wakasirishwa’ na Sifuna kwa ‘kuyumbisha’ ODM
WANACHAMA wa UDA wanadai kuwa mgawanyiko unaoshuhudiwa katika chama cha ODM umesababishwa na aliyekuwa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta na viongozi wengine ambao hawataki muungano wa chama tawala na chama cha chungwa.
Aidha, chama cha Rais William Ruto kimesema nia ya upinzani ni kuhujumu serikali ya sasa. Hata hivyo, chama tawala kimesema kiko tayari kumenyana na wapinzani wao katika kura za mwaka 2027.
Wakiongozwa na Katibu Mkuu Bw Hassan Omar, wanasiasa hao walisema nia yao ni kutafuta muungano na chama cha ODM ili kushinda uchaguzi wa mwaka ujao na kuunda serikali ya pamoja.
Hata hivyo, walisema kikwazo kikubwa kimeletwa na Bw Kenyatta.
“Hatuwezi kukubali, Bw Kenyatta, Gavana James Orengo (Siaya) na Seneta Edwin Sifuna. Hao wote tutawaweka katika kaburi la sahau. Wale wako ODM na hawataki kuendelea na safari ya Rais Ruto ni vikaragosi ambao wamelipwa na wafadhili kutoka Mlima Kenya ili kutatiza serikali ya Kenya Kwanza,” alisema Bw Omar.
Viongozi hao wa UDA walisema wanasiasa wa mrengo wa ODM unaoongozwa na Gavana Orengo, Seneta Sifuna miongoni mwa viongozi wengine, ni wa kulemaza mpango wa kuiunganisha chama cha UDA na ODM kwa ajili ya uchaguzi ujao.
Gavana wa Lamu Bw Issa Timammy aliwasihi wapwani kujiandikisha kama wapigakura ili kuzoa kura nyingi kwenye uchaguzi mkuu wa 2027.
“Tujiandikisha katika kila kituo cha kupiga kura kwa wingi kama wapiga kura na kuiunga mkono azma ya Rais Ruto kuwania urais kwa mara ya pili. Tutafanyiwa chochote tutakacho na Rais atakapoingia mamlakani kwa awamu ya pili,” alisema.
Gavana wa Kwale Bi Fatuma Achani, alisema na Mbunge wa Msambweni Bw Feisal Bader, waliwasihi wakazi kuunga chama tawala ili wafaidike zaidi na serikali ijayo.
Seneta wa Tana River, Bw Danson Mungatana alisema UDA imepania kuzoa viongozi wengi kwenye uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
“Tunataka tuongeze maseneta, magavana na wabunge. Kati ya maseneta sita wa eneo la Pwani kutoka Kwale, Kilifi, Lamu, Taita Taveta, na Tana River mimi tu ndio nilichaguliwa kupitia chama cha UDA. Katika upande wa magavana Bi Achani ndiye wa UDA eneo nzima la Pwani,” alisema Bw Mungatana.
Bw Mungatana alisema Bi Achani si mfisadi akimpigia debe awamu ya pili. Vile vile aliwasihi viongozi wa UDA kushirikiana na ODM ili kuzoa kura nyingi kwa Rais Ruto.
Hata hivyo alisema UDA itasimamisha viongozi katika viti vyote vya kisiasa ili kuwe na ushindani na kuzuia wapinzani kupenya kwenye debeni.
Aliwasihi wapinzani wa Bi Achani kumpa nafasi kumaliza muhula wa pili na badala yake kupigania viti vyengine kama useneta na ubunge.
“Ninataka kuwaambia wapinzani wa Bi Achani, mnapiganaje na mwanamke? Si mumwachie amalize muhula wa pili? Mwacheni amalize muhula wake,” alisema.