DPP wapata pigo korti ikikataa kufungua upya kesi ya Mackenzie
OFISI ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) imepata pigo baada ya Mahakama Kuu jijini Mombasa kutupilia mbali ombi lake la kufungua upya kesi ya mauaji ya watoto 191 dhidi ya mhubiri mashuhuri Paul Mackenzie na washukiwa wenzake 29.
Mahakama ilikataa ombi la upande wa mashtaka, ikibainisha kuwa ingawa ina mamlaka ya kuitisha mashahidi kurudi kutoa ushahidi pale ushahidi wao unapokuwa muhimu kufanikisha uamuzi wa haki, mamlaka hiyo haiwezi kutumika kusaidia kujaza mapengo, kurekebisha mapungufu au kuimarisha kesi baada ya kufungwa kwa hiari.
“Ikizingatiwa kuwa ombi hili limewasilishwa kama jaribio la kurekebisha kosa la kisheria kwa manufaa ya washukiwa, kwa hakika ni mbinu ya upande wa mashtaka kusaidia kujaza mapengo katika kesi yake kupitia uchunguzi mpya wa mtuhumiwa,” jaji alisema.
Upande wa mashtaka ulikuwa unataka Enos Amanya aitwe tena mahakamani kwa ajili ya kuulizwa maswali kuhusu ushahidi wake wa kukiri kilichochochea matukio mauaji ya Shakahola.
Hata hivyo, mahakama ilibainisha kuwa Amanya hakuwa shahidi wa upande wa mashtaka katika kesi kuu, na kukiri kwake si ushahidi wa msingi unaoweza kusababisha washukiwa wenzake kupatikana na hatia bila kutegemea ushahidi huru.
“Kwa kuzingatia hali hii, ombi hili halina msingi na halina manufaa,” Jaji alisema.
Mnamo Januari 22, upande wa mashtaka uliomba kufungua kesi hiyo ili kuruhusu Mackenzie na wenzake 29, ambao bado wamekana mashtaka dhidi yao, kuwa na nafasi ya kumuuliza maswali Amanya kuhusu kukiri alikokurekodi Januari 16, 2026.
Ombi hilo liliwasilishwa baada ya upande wa mashtaka kufunga kesi yake kwa kuwasilisha mashahidi 119 kuunga mkono mashtaka 191.
Amanya, mwenye umri wa miaka 51, aliyekuwa mkuu wa usalama wa Msitu wa Shakahola, alibadilisha hoja yake mwanzoni mwa mwaka huu, akikiri mashtaka 191 ya mauaji na kurekodi maelezo yake kwa kina kilichotokea msituni, jukumu lake na la wengine kati ya 2021 na 2023.