Dimba

Presha ya Arsenal kulaza Wolves leo na ‘kuregesha ujumbe’ kwa Man City

Na MASHIRIKA February 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

LONDON, Uingereza

VINARA wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), Arsenal wanapania kufungua mwanya wa alama saba kileleni mwa jedwali, watakapomenyana na Wolves leo ugani Molineux kuanzia saa tano usiku.

Arsenal ambao pia wako mbioni kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), katika mechi ya mkondo wa kwanza ugani Emirates mnamo Desemba , walinusurika kichapo hata baada ya kupata ushindi wa mabao 2-1.

Vijana wa Mikel Arteta waliponea pambano hilo huku Wolves wakifunga mabao yote matatu (yakiwemo mawili ya kujifunga).

Wachezaji wa Wolves Sam Johnstone na Yerson na Mosquera walijifunga huku Tolu Arokodare akifungia Wolves bao la kufutia machozi.

Katika mechi hiyo, Arsenal walikuwa bora. Walilenga shabaha mara tano, ikiwa zaidi ya maradufu ikilinganishwa na Wolves (mara mbili). Pia walimiliki mpira asilimia 70 ikilinganishwa na wageni wao hao (asilimia 30).

Gunners wanatarajiwa kutumia motisha ya Jumapili ya kufuzu raundi ya tano ya Kombe la FA kwa mara ya kwanza tangu 2020, kutokana na ushindi wa 4-0 Wigan Athletic.

Msimu huo huo, Arteta alishinda kombe hilo ambalo ndilo kombe la pekee aliloshinda hadi sasa kama kocha wa timu hiyo.

Sambamba na Arsenal, Wolves pia waliingia katika raundi ya tano ya kombe hilo, baada ya ushindi finyu wa 1-0 dhidi ya Grimsby Town 1-0 mnamo Jumapili, bao lililotiwa kimiani na Santiago Bueno kipindi cha pili.

Hata hivyo, Arteta ataendelea kupambana katika mechi moja baada ya nyingine, huku kibarua cha kushinda Kombe la FA, Kombe la Carabao na Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya kikimsubiri.

Arsenal wamepoteza mechi moja tu kati ya 11 za EPL msimu huu. Wamepata ushindi mara saba na kupoteza mechi tatu, lakini sare ya 1-1 dhidi ya Brentford wiki iliyopita iliwaweka pabaya katika mbio za kutwaa taji la EPL.

Safari ngumu ya kuelekea Etihad hapo Aprili inawasubiri, lakini sare hiyo imewaruhusu wapinzani wao Manchester City kupunguza pengo hadi alama nne, zikiwa zimesalia mechi 12 msimu kukamilika.

Arsenal wako kileleni mwa jedwali kwa alama 57. Wameshinda mechi tisa kati ya 11 za EPL dhidi ya Wolves na kupoteza mechi mbili, kikiwa kiwango chao cha juu zaidi cha ushindi dhidi ya timu yoyote ile.

Wolves wanasalia kuburura mkia wakiwa na alama tisa pekee. Timu hiyo imepoteza mechi 10 kati ya 13 za nyumbani za EPL msimu huu (ushindi mmoja, sare mbili).