Jinsi mtandao wa kijamii umemfungulia soko la kuku na vifaranga
ALIPOKUWA bado shuleni miaka kadhaa iliyopita, Lucy Ichuga alipenda kilimo, akiwa na shauku ya kuwa mfugaji wa kuku.
Baada ya ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa 2007, Ichuga alianza kuuza vitunguu kwa jumla katika soko la Molo katika Kaunti ya Nakuru.
“Mwishoni mwa 2019, nilisoma chapisho lililohusisha mkulima aliyekuwa akiuza vifaranga vyake mtandaoni. Nilipompigia simu, niligundua kuwa alikuwa mkulima kutoka eneo langu, na kwa hivyo, ilikuwa rahisi kupata vifaranga kutoka kwake,” anasema Ichuga, akiongeza kuwa wakati wa amri ya kutotoka nje kote nchini iliyowekwa na serikali kufuatia mlipuko wa virusi vya corona, alijenga jengo la muda na kununua vifaranga 80 kwa Sh350 kila kimoja.
Wakati wa mahojiano nyumbani kwake katika mji wa Molo hivi majuzi, Ichuga alisema baada ya miezi miwili na nusu, kuku walianza kutaga mayai.
Alipotangaza mayai na kuku mtandaoni, alikutana na kuzungumza na mkulima ambaye alimwonyesha jinsi ya kulea vifaranga.
Anasema kuwa alipendezwa na jambo hilo na kuendelea kujifunza mtandaoni.
Katika mwaka huo huo, aliamua kujenga jengo la kisasa na kubwa ambalo lingewatosha kuku na kuwa na nafasi ya kutosha kulea vifaranga wake kwa urahisi.
Kwa Sh350,000 alizokuwa nazo kama mtaji, Ichuga alinunua mahitaji ya ujenzi na vyombo vilivyohitajika kufugia kuku.
Aligawanya nyumba hiyo katika vyumba vitano ambavyo vingeweza kubeba kuku na vifaranga zaidi ya 500 waliokomaa.
Kama mfanyabiashara, alikuwa ametenga Sh70,000 za ziada ambazo alisema zilitosha kununua vifaranga 70, mmoja akiuzwa kwa Sh100.
“Baada ya kuwalea vifaranga wangu kwa mwezi mmoja, niliendelea kuwalisha na kufikia mwisho wa miezi minne na nusu, walikuwa tayari kutaga mayai. Katika mchakato huo, niliuza majogoo waliokomaa kwa kati ya Sh1,400 na Sh1,500 mtawalia kulingana na ukubwa,” anasema Ichuga, na kuongeza kuwa aliuza mayai yake katika soko la ndani kwa Sh15 kila moja.
Anasema kuwa mayai yalikuwa mengi na ilikuwa changamoto kuyauza kwa sababu wateja walikuwa wachache na hii ilisababisha mrundikano mkubwa wa mayai. Hapa, aliamua kuuza kuku waliokomaa kupitia mitandao ya kijamii.
Uzito
Mnamo 2021, aligundua kuwa kuku wake wa kienyeji walioboreshwa waliongeza uzito na baadhi yao walikufa kutokana na msongamano ndani ya vyumba.
Anasema soko halikuwa lizuri na wateja wachache waliokuja kununua kuku wake walitaka kununua kwa bei ya chini bila kujua changamoto aliyokumbana nayo, hasa kutumia pesa nyingi kuwalisha. Anaongeza kuwa kuku aliyekomaa angekula gramu 140 ama 150 kila siku.
Mkulima huyo anaeleza kuwa msimu huo wa corona uliathiri ufugaji wake wa kuku.
Aliuza kundi lake lote na akaacha kununua vifaranga kwa sababu hakukuwa na soko tayari la kuuza kuku wake.
Baada ya miezi michache na nyumba ya kuku kukaa tupu, alianzisha tena biashara yake baada ya maafisa kutoka kampuni fulani kumtembelea na kujitolea kumpa vifaranga vya siku moja pamoja na wakazi wengine ambao walikuwa wameunda vikundi katika jamii ili wawalee na kuwauza.
Kuanzia 2022 hadi sasa, akawa mtaalamu wa kuwalea vifaranga. Pia, wakulima na kampuni zingine zilimfikia kwa ushauri zaidi.
“Miezi kadhaa baada ya kuacha ufugaji wa kuku, baadaye nilifanikiwa katika jaribio langu la pili nilipoamua kuanza kuuza vifaranga vya mwezi mmoja kwa Sh300 kila kimoja kwa sababu hawakuwa wakila sana. Tofauti na kuku waliokomaa ambao walikula sana, biashara ilikuwa bora zaidi kwa sababu vifaranga walikula chakula kidogo,” anaeleza Ichuga, akiongeza kuwa hutembea kwa maonyesho ya kilimo, hutangamana na wakulima wenye uzoefu na kufanya utafiti mtandaoni ili kuongeza ujuzi wake.
Kwa sasa, mkulima ana takriban vifaranga 500 na zaidi ya kuku 200. Anauza vifaranga vyake vya wiki tatu hadi tano kwa kati ya Sh300 na Sh350 mtawalia.
Mkulima huyu anayepata vifaranga wake kutoka kwa kampuni tofauti zilizoopendekezwa, anasema amepata wateja zaidi kupitia mtandao, akiongeza kuwa kupitia chanjo, malisho bora, kukabili minyoo baada ya kila miezi miwili miongoni mwa mengine, kumechangia pakubwa kudumisha na kupata wateja zaidi.
Ili kuhakikisha kwamba vifaranga wake wapya wako salama, yeye hudumisha usafi na kuua vijidudu vya kuku kabla ya kuleta vifaranga wapya ili kuzuia magonjwa kama vile coccidiosis.
Mkulima anasema kinyesi cha kuku kinahitajika sana katika eneo hilo. Kwa upande wake, anakitumia kama mbolea shambani mwake na anauza ya ziada kwa wakulima wengine kwa Sh500 katika kila mfuko wa kilo 90.
Anataja ukosefu wa ujuzi wakati wa kutafuta vifaranga wanaopendekezwa, malisho sahihi na bora na mrundikano wa uzalishaji wa mayai miongoni mwa mengine kama changamoto kuu wakati wa mchakato wa kutaga.
Ichuga sasa anawekeza kikamilifu katika kuku 250 wa kutaga mayai.
Anasema hawali chakula kingi ikilinganishwa na kuku wa kienyeji walioboreshwa.
“Mpango wangu ni kujenga banda jingine kubwa la kuku ambapo nitaweka kuku zaidi wa kutaga mayai ninapoendelea na mradi wangu wa vifaranga. Nina matumaini ya kuwa na zaidi ya 1,000 ifikapo mwaka ujao,” anasema, huku akiongeza kuwa biashara ya mayai ni nzuri kwa soko na yanauzwa kwa Sh20 kila moja, trei ya mayai 30 ikiuzwa kwa Sh 600.
Wakati mahitaji ya vifaranga na kuku yanapoongezeka, Ichuga hutafuta kutoka kwa wakulima wengine ili kuwaridhisha wateja wake, haswa kati ya Agosti na Desemba.
“Kuweka kumbukumbu kumenisaidia kuendeleza mradi wangu na kupanda mazao shambani na hii imenifanya nifanikiwe. Ninawasihi wakulima kuunda vikundi ili kunufaika na vifaa vya serikali,” anaongeza Ichuga.