Wakuu wa shule wapendekeza karo iongezwe
HUENDA wazazi wakalazimika kulipa karo ya juu zaidi kwa watoto wao wanaosoma katika shule za upili za umma ikiwa mapendekezo mapya ya wakuu wa shule yatapitishwa na serikali.
Wakuu hao wa shule wanasema muundo wa sasa wa karo ulipitiwa mara ya mwisho mwaka wa 2015 na hauendani tena na hali ya sasa ya uchumi, mfumuko wa bei na kupanda kwa gharama ya maisha.
Mapendekezo hayo yaliwasilishwa kwa Katibu wa Elimu ya Msingi Dkt John Ololtuaa, wakati wa mkutano wa mwaka wa Chama cha Wakuu wa Shule za Upili Kenya (KESSHA) uliofanyika Mombasa.
Kwa mujibu wa KESSHA, serikali imekuwa ikitoa fedha za ufadhili wa elimu kwa viwango vya chini kuliko ilivyoidhinishwa.
Ingawa kila mwanafunzi anapaswa kupata Sh22,244 kupitia mpango wa Elimu ya Kutwa ya Sekondari Bila Malipo (FDSE), kiasi kinachotolewa kimeendelea kupungua na kufikia Sh15,385.12 katika mwaka wa kifedha wa 2024/2025.
Hali hiyo, wakuu wa shule wanasema, imewaacha na madeni makubwa pamoja na mishahara ya wafanyakazi wasio walimu ambao hawajalipa.
KESSHA inakadiria kuwa serikali haijatoa jumla ya Sh22.5 bilioni zilizostahili kutumwa shuleni mwaka huu pekee. Chini ya mapendekezo hayo mapya, wazazi walio na watoto katika shule za kitaifa watalipa Sh87,781 kwa mwaka baada ya kuondolewa kwa ufadhili wa serikali.
KESSHA inasema gharama halisi ya kuhudumia mwanafunzi katika shule ya bweni ya kitaifa imefikia Sh110,025 kwa mwaka.
Katika shule za kaunti ndogo na za mikoa, karo iliyopendekezwa ni Sh83,622 kwa mwaka kwa kila mwanafunzi.
Shule za kutwa za kaunti nazo zinapendekezwa kutoza Sh7,675 kwa mwaka baada ya ufadhili wa serikali.
Mwenyekiti wa kitaifa wa KESSHA, Bw Willy Kuria, alisema mfumo wa sasa wa karo ulianzishwa mwaka wa 2015 na hauwezi tena kuhimili gharama za kuendesha shule.
Alisema bei za bidhaa na huduma muhimu zimeongezeka pakubwa katika kipindi hicho, huku thamani ya shilingi ya Kenya ikishuka.