Ujenzi wa Thika Stadium waanza AFCON ikinukia
SERIKALI imetoa hakikisho kwamba hakuna uhamishaji au usumbufu wa shughuli za biashara utakaotokea wakati wa ujenzi wa uwanja wa Manisipaa ya Thika katika Kaunti ya Kiambu.
Uwanja huo unatarajiwa kuchukua chini ya mwaka mmoja kukamilika kwa matarajio ya kutumika kama sehemu ya mazoezi wakati wa michuano ya Kombe la Afrika (AFCON) mwakani.
Kenya itakuwa mwenyeji wa AFCON 2027 pamoja na Uganda na Tanzania.
Akizuru uwanja huo mnamo Jumatatu, Waziri wa Michezo Salim Mvurya alisema ujenzi wa uwanja huo ambao una uwezo wa kubeba mashabiki 10,000, utatumika kukuza vipaji chipukizi katika kaunti hiyo.
“Wafanyabiashara wadogo wadogo kutoka eneo hili hawatasumbuliwa kwa vyovyote wakati wa ujenzi wa uwanja huu,” alisema Mvurya.
Mvurya alikuwa ameandamana na mwenzake wa Ulinzi, Soipan Tuya, Katibu wa Michezo Elijah Mwangi na Katibu katika Wizara ya Ulinzi Patrick Mariru.
Aidha, Mvurya alieleza kuwa ujenzi wa uwanja huo ulikuwa ni msukumo mkubwa kutoka kwa serikali ya Kaunti katika uanzishaji wa miundomsingi ya kimkakati ambayo itakuza shughuli za biashara na uchumi.
Hakikisho la Waziri lilituliza wasiwasi na hofu ya wafanyabiashara na viongozi wa eneo hilo ambao walitaka kujua hatima ya wafanyabiashara walio karibu na uwanja huo mara tu mradi huo utakapoanza.
Kauli ya Mvurya yaliungwa mkono na Waziri Tuya ambaye alisema kuwa hata uwanja wa mpira wa kikapu na bwawa la kuogelea pia vitakarabatiwa.
“Huduma zilizowekwa katika uwanja huo ili kukuza michezo hazitaathiriwa na ujenzi wa uwanja,” alisema Tuya.
Mbali na uwanja huo kutumika kucheza soka, pia wanariadha watautumia kufanyia mazoezi yao.
Pia, kutajengwa vyumba vya kubadilishia nguo na sehemu ya watu mashuhuri.
Bw Mwangi alifichua kuwa Kaunti ya Kiambu ni kati ya maeneo yatakayonufaika pakubwa kutokana na mpango unaoendelea wa serikali wa kujenga viwanja.
Kaunti ya Kiambu ni nyumbani kwa viwanja vitatu vikuu vinavyojumuisha Kirigiti, Karatu na Thika.